1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

BEIRUT: Maelfu wa wapalestina wakimbia kambi ya wakimbizi

23 Mei 2007
https://p.dw.com/p/CBzE

Maelfu ya watu wamekuwa wakikimbia kutoka kambi ya wakimbizi iliyo kaskazini mwa Lebanon kufuatia siku tatu za mapigano makali kati ya vikosi vya usalama na wanamgambo wa kiislamu.

Wakaazi wa kipalestina kwenye kambi ya Nahr al Bared walikwama ndani ya kambi hiyo wakati wanajeshi walipokuwa wakikabiliana na wapiganaji wa kundi la Fatah al Islam walio ndani ya kambi hiyo.

Walioshuhudia wanasema wakaazi wengi wametumia muda mfupi yaliposita mapigano kukimbia, baada ya usitishwaji mapigano kutangazwa rasmi.

Mjumbe wa Umoja wa Mataifa aliyepeleka misaada katika kambi ya wakimbizi alisema walishambuliwa wakati walipokuwa wakigawa misaada.

´Wakati wa kugawa chakula kwenye barabara kuu kambini, tulishambuliwa kwa risasi na magari yetu yakalengwa. Tuna magari manne kambini ambayo hatuwezi kuyatoa.´

Kundi la Fatah al Islam lililo na mafunganao na kundi la al-Qaeda, ambalo limekuwa likipambana na vikosi vya jeshi la Lebanon, limesema litaheshimu amri ya kusitisha mapigano lakini likaapa wapiganaji wake hawatajisalimisha.

Sambamba na taarifa hiyo, afisa wa chama cha PLO amesema hii leo kwamba chama hicho hakitapinga ikiwa jeshi la Lebanon litaamua kutuma wanajeshi wake kwenda katika kambi ya wakimbizi ya Nahr al Bared kuwachakaza wanamgambo hao wa kiislamu.