1. Inhalt
  2. Navigation
  3. Weitere Inhalte
  4. Metanavigation
  5. Suche
  6. Choose from 30 Languages
Matangazo
Matangazo
Matangazo
HABARI

Habari za Ulimwengu | 13.05.2022 | 13:00

G7 yaahidi kuisaidia Ukraine hadi ipate ushindi

Mawaziri wa mambo ya nje wa kundi la nchi saba zilizoendelea zaidi kiuchumi duniani, G7, wameahidi kuisaidia Ukraine katika vita vyake na Urusi, huku Umoja wa Ulaya ukiahidi kuongeza msaada kwa Ukraine kwa zaidi ya dola nusu bilioni. Mawaziri hao wamekutana leo katika mkutano wao wa siku tatu nchini Ujerumani. Waziri wa Mambo ya Nje wa Ufaransa, Jean-Yves Le Drian amesema kundi la G7 limeungana zaidi katika nia yao ya kuendelea kwa muda mrefu kuisaidia Ukraine kupigania uhuru wake hadi itakaposhinda. Mkuu wa sera za kigeni wa Umoja wa Ulaya, Josep Borrell, amesema umoja huo umeahidi kutoa euro milioni 500 zaidi kama msaada wa kijeshi kwa Ukraine. Fedha hizo zitaongeza jumla ya msaada uliotolewa na Umoja wa Ulaya kwa Ukraine na kufikia euro bilioni mbili.

Scholz na Putin waijadili Ukraine

Kansela wa Ujerumani, Olaf Scholz, na Rais wa Urusi, Vladmir Putin, wamejadiliana kuhusu hali ya Ukraine wakati walipozungumza leo kwa njia ya simu. Ikulu ya Urusi imesema hayo yalikuwa mazungumzo ya kwanza ya simu baina ya viongozi hao wawili baada ya kutozungumza kwa wiki kadhaa, juhudi zilizoanzishwa na Ujerumani. Kansela Scholz amemtaka Rais Putin kukubali kusitisha mapigano nchini Ukraine haraka iwezekanavyo. Msemaji wa serikali ya Ujerumani amesema makubaliano yanahitajika ili kuimarisha hali ya kiutu nchini Ukraine na kuruhusu maendeleo katika kutafuta ufumbuzi wa kidiplomasia kwa mzozo huo. Wakati wa mazungumzo yao yaliyodumu kwa dakika 75, Scholz amemkumbusha Putin kuhusu jukumu la Urusi kutokana na hali ya chakula iliyopo sasa ulimwenguni.

Uturuki yapinga Finland na Sweden kujiunga NATO

Rais wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan amesema nchi yake haiafikiani na nia ya Finland na Sweden kutaka kujiunga na Jumuia ya Kujihami ya NATO. Akizungumza leo na waandishi habari mjini Istanbul, Erdogan amedai nchi hizo za Scandnavia ni maficho ya makundi ya kigaidi. Kwa muda mrefu, Uturuki imekuwa ikizishutumu nchi za kanda ya Nordic, hasa Sweden ambayo imekuwa na jumuia kubwa ya wahamiaji wa Kituruki, kwa kuyahifadhi makundi ya Kikurdi yenye msimamo mkali pamoja na wafuasi wa Fethullah Gulen, muhubiri anayeishi Marekani anayehusishwa na jaribio la mapinduzi la mwaka 2016. Wakati huo huo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Finland, Pekka Haavisto, amehimiza kuwepo uvumilivu na ametoa wito wa kushughulikiwa hatua kwa hatua upinzani unaofanywa na Uturuki dhidi ya Finland na Sweden kujiunga na NATO.

Israel yatangaza matokeo ya awali ya uchunguzi wa kifo cha mwandishi wa Al Jazeera

Matokeo ya uchunguzi wa awali wa jeshi la Israel yameonyesha kuwa haijulikani ni nani aliyemuua kwa kumpiga risasi mwandishi habari wa kituo cha televisheni cha Al Jazeera, Shireen Abu Akleh, katika Ukingo wa Magharibi. Shireen alipigwa risasi siku ya Jumatano wakati akiripoti kuhusu uvamizi wa jeshi la Israel. Jeshi hilo limesema hitimisho kutoka kwenye ripoti ya muda imeonesha kuwa haijaweza kubaini chanzo cha risasi ambazo zilimuua Shireen. Ripoti hiyo imesema uchunguzi unaonesha uwezekano wa aina mbili wa chanzo cha risasi iliyomuua. Wa kwanza inawezekana risasi zilizofyatuliwa na raia wa Kipalestina aliyekuwa na bunduki dhidi ya wanajeshi wa Israel, kama sehemu ya mamia ya risasi zilizorushwa kutoka kwenye maeneo tofauti. Na wa pili ni kwamba wakati wa kurushiana risasi, mwanajeshi mmoja alifyatua risasi kutoka kwenye gari kwa kutumia darubini dhidi ya gaidi aliyekuwa akilifyatulia risasi gari hilo.

Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu afariki dunia

Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu, Sheikh Khalifa bin Zayed Al-Nahyan, amefariki dunia akiwa na miaka 73, baada ya kuugua kwa miaka kadhaa. Kuna uwezekano nafasi ya Sheikh Khalifa ambaye hakuwa akionekana sana hadharani, ikachukuliwa na kaka yake mrithi wa kiti cha ufalme wa Abu Dhabi, Mohammed bin Zayed, ambaye tayari alikuwa akionekana kama mtawala mkuu wa Falme hizo za Kiarabu. Wizara inayohusika na masuala ya rais imetangaza siku 40 za maombolezo, huku bendera zikipepea nusu mlingoti kuanzia leo na kusitishwa kwa kazi katika sekta ya umma na binafsi kwa siku tatu za mwanzo. Sheikh Khalifa alichukua madaraka Novemba mwaka 2004, akimrithi baba yake kama mtawala wa 16 wa Abu Dhabi, ambayo ni tajiri zaidi kati ya Falme saba za shirikisho hilo. Rais wa Marekani, Joe Biden ametuma salamu za rambirambi kwa Umoja wa Falme za Kiarabu kufuatia kifo hicho.

Chama kikuu cha upinzani Sri Lanka chajiunga na maandamano

Chama kikuu cha upinzani nchini Sri Lanka leo kimeungana na maandamano ya kuipinga serikali kukataa uteuzi wa waziri mkuu mpya. Badala yake chama hicho kinasisitiza rais ajiuzulu kutokana na mzozo mbaya wa kiuchumi ulioikumba nchi hiyo. Jana, Rais Gotabaya Rajapaksa alimteua Ranil Wickremesinghe aliyewahi kuwa waziri mkuu mara tano, kushika wadhifa huo kwa mara ya sita, lakini upinzani umesema hilo halitasuluhisha mzozo wa kisiasa na kiuchumi nchini humo. Kaka wa Gotabaya, Mahinda Rajapaksa, alijiuzulu nafasi yake ya waziri mkuu siku ya Jumatatu wakati ambapo ghasia zikisambaa na amejificha katika kambi ya jeshi. Eran Wickramaratne, mwanachama mwandamizi wa chama kikuu cha upinzani cha Samagi Jana Balawegaya, amesema wanataka familia ya Rajapaksa iondoke kabisa madarakani. Leo, waziri mkuu mpya wa Sri Lanka alikutana na mabalozi wanaoziwakilisha nchi za India, Japan, Marekani na China.

Korea Kusini kuisaidia Korea Kaskazini kwa chanjo ya COVID-19

Ofisi ya Rais wa Korea Kusini, Yoon Suk-yeol imesema leo kuwa inakusudia kuipatia Korea Kaskazini chanjo za COVID-19 na vifaa vingine vya matibabu, siku moja baada ya jirani yake huyo kutangaza mripuko wa kwanza wa virusi vya corona. Msemaji wa Rais Yoon, amesema Korea Kusini itajadiliana kwa undani mipango ya msaada huo na Korea Kaskazini. Hatua hiyo imefikiwa baada ya Korea Kaskazini kukumbwa na mripuko wa kwanza wa COVID-19, bila kuwa na mpango wa chanjo unaojulikana, na hivyo kuibua wito mpya kwa serikali kukubali msaada utakaokoa maisha ya watu. Maafisa wa Korea Kusini wamesema Korea Kaskazini haitaki chanjo za Sinovac wala Astrazeneca na badala yake inapendelea chanjo zilizotengenzwa na kampuni za madawa ya Marekani za Moderna na Pfizer. Jana, Marekani ilisema itaunga mkono kuisaidia Korea Kaskazini, lakini kwa sasa haina mipango ya kugawa chanjo hizo.

MATUKIO YA KISIASA
MATUKIO YA AFRIKA
MASUALA YA JAMII
MICHEZO
HABARI KWA LUGHA YA KIINGEREZA

Matangazo
Tazama vidio 02:23

Vidio zaidi

Wafahamu vijana wanaharakati wa mazingira Ghana

Wafahamu vijana wanaharakati wa mazingira Ghana

Ulaya kuipatia Ukraine msaada wa euro milioni mia tano

Ulaya kuipatia Ukraine msaada wa euro milioni mia tano

Kutana na wasichana wanasoka chipukizi Tanzania

Kutana na wasichana wanasoka chipukizi Tanzania

Kituo cha radio kwa wasanii wasio na makazi Kenya

Kituo cha radio kwa wasanii wasio na makazi Kenya

TUFUATILIE KATIKA MITANDAO YETU YA KIJAMII