1. Inhalt
  2. Navigation
  3. Weitere Inhalte
  4. Metanavigation
  5. Suche
  6. Choose from 30 Languages
Matangazo
Matangazo
Matangazo
HABARI

Habari za Ulimwengu | 15.03.2022 | 14:00

Rais wa Ukraine aomba msaada zaodo wa silaha kutoka Ulaya

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky ameomba msaada wa silaha zaidi kutoka Ulaya na amesema viongozi wa nchi za Ulaya ya kaskazini watakuwa wanajisaidia wenyewe ikiwa wataisaidia Ukraine. Zelensky ameeleza kuwa anahitaji silaha zaidi ili kuzuia uvamizi wa Urusi. Akitoa wito huo kwa njia ya video Zelensky amesema jeshi lake linatumia na kuzimaliza haraka silaha ambazo nchi za magharibi zinapeleka Ukraine. Pia ametoa wito wa kuweka vikwazo vyote vya kibiashara dhidi ya Urusi na kusema kuwa vikwazo vya hadi sasa havitoshi kuyazuia majeshi ya Urusi yanayosonga mbele. Amesema inapasa kutambua kwamba Urusi ni nchi isiyojali sheria za kimataifa. Rais huyo ya Ukraine kwa mara nyingine ameelezea masikitiko yake juu ya uamuzi wa nchi za NATO wa kukataa kuilinda anga ya Ukraine. Rais huyo wa Ukraine alikuwa anazungumza na kundi la JEF, la nchi 10 za NATO, eneo la Baltik na za Ulaya magharibi. Kundi hilo linashughulikia migogoro ya kimataifa.

Mazungumzo kati ya urusi na Ukraine yaendelea

Mazungumzo ya kumaliza vita kati ya Ukraine na Urusi yanaendelea leo Jumanne. Hayo ni kulingana na kiongozi wa ujumbe wa Ukraine David Arachamiya aliyenukuliwa na gazeti moja la nchini humo ingawa hakutoa maelezo zaidi. Urusi haijatoa maelezo yoyote kuhusiana na mkutano huo. Pande zote mbili zilikutana jana Jumatatu kwa njia ya video katika duru ya nne ya mazungumzo na kisha baadaye mchana mshauri wa rais wa Ukraine Mykhailo Podolyak alitangaza kuwa mazungumzo hayo yameahirishwa hadi leo Jumanne. Ukraine inataka vita visimamishwe na pia kuondolewa askari wote wa Urusi kutoka nchini humo. Urusi nayo inaitaka Ukraine itambue jimbo la Crimea lililotwaliwa na Urusi katika rasi ya Bahari Nyeusi kama eneo halali ya Urusi.

Kansela wa Ujerumani asifu safari ya mawaziri wakuu watatu nchini Ukraine

Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz amepokea kwa furaha hatua ya mawaziri wakuu wa Poland, Jamhuri ya Czech na Slovenia ya kufanya safari mjini Kiev leo Jumanne, akisema ni vizuri kutumia njia tiofauti za kutafuta suluhisho la mzozo wa Ukraine na Urusi. Kansela Scholz amesema jumuiya ya kimataifa inafuata mkakati wa wazi wa kisiasa kuisaidia Ukraine. Scholz amesema njia zote za kidiplomasia zinapaswa kutumika katika kutafuta suluhu ya mgogoro wa Ukraine na kuhimiza kusitishwa kwa mapigano mara moja. Kansela wa Ujerumani amesema ni muhimu kuendelea na majadiliano na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky na pia Rais wa Urusi Vladimir Putin, ili kufanikisha makubaliano ya kusitisha mapigano.

UNHCR yasema michango kwa ajili ya Ukraine imevunja rekodi

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuwahudumia wakimbizi UNHCR limesema kiasi cha michango ya dharura kwa ajili ya kuisaidia Ukraine kimevunja rekodi. Shirika hilo limesema makampuni, wakfu na wafadhili mbalimbali wamechangia zaidi ya dola milioni 200 katika muda wa wiki mbili kwa ajili ya Ukraine. Kamishna Mkuu wa Umoja wa Mataifa anayesimamia huduma kwa wakimbizi Filippo Grandi amewashukuru wote walochangia duniani kote kwa wema na ukarimu wao wa kuwasaidia watu wanaokimbia vita nchini Ukraineambapo mamilioni ya watu wanahitaji msaada wa haraka. Idadi ya watu walioikimbia Ukraine tangu Urusi ilipoivamia nchi hiyo imezidi watu milioni 2.8. Kulingana na shirika la UNHCR, zaidi ya watu milioni 2 wamegeuka kuwa wakimbizi wa ndani.

Iran yaitaka Marekani iamue juu ya kuurejesha mkataba wa nyuklia

Wizara ya mambo ya nje ya Iran imesema Marekani inapaswa kuamua juu ya kuurejesha mkataba wa nyuklia uliofikiwa mnamo mwaka 2015 baina ya nchi hiyo na mataifa makubwa huku ukiwepo wasi wasi juu ya mazungumzo ya mjini Vienna kuvunjika. Juhudi za kufikia mapatano zimeingia katika hali ya sintofahamu baada ya Urusi, kutoa masharti katika dakika ya mwisho. Urusi kwa sasa inazozana na nchi za magharibi baada ya kuivamia Ukraine. Mazungumzo yamesimamishwa kwa muda usiojulikana licha ya hati husika kukamilika. Waziri wa mambo ya nje wa Urusi Lavrov amekanusha madai ya Marekani kuwa Urusi inayakwamisha mazungumzo ya mjini Vienna juu ya kuufufua mkataba na Iran. Waziri huyo amesema Urusi inataka mkataba huo urejeshwe haraka lakini inasubiri Marekani iondoe vikwazo ilivyoweka dhidi ya Iran.

Nchi za Ghuba kuandaa mazungumzo juu ya vita vya nchini Yemen

Nchi za Ghuba zinakusudia kuandaa mazungumzo kati ya pande zote zinazohusika na mgogoro wa nchini Yemen ikiwa pamoja na wajumbe wa Kihouthi wanaoungwa mkono na Iran. Mazungumzo hayo yatafanyika mjini Riyadh mwishoni mwa mwezi huu. Baraza la ushirikiano wa nchi sita za Ghuba limesema lengo la mazungumzo hayo ni kuvimaliza vita vya wenyewe kwa wenyewe vya nchini Yemen viliavyoanza tangu mwaka 2015. Mjumbe mmoja wa serikali ya Yemen inayoungwa mkono na Saudi Arabia ameeleza kuwa upande wao upo tayari kuhudhuria mkutano huo ili kutafuta suluhisho juu ya masuala ya usalama, kisiasa na kijeshi. Hata hivyo ameelezea wasi wasi iwapo waasi wa Houthi watakubali kuhudhuria mazungumzo hayo katika mji mkuu wa Saudi Arabia ambayo inaongoza mfungamano wa kijeshi ili kuisaidia serikali ya Yeman kupambana na waasi hao. Saudi Arabia haitashiriki kwenye mazungumzo hayo endapo yatafanyika.

Umoja wa Mataifa wasema dalili zaonyesha jeshi la Myanmar limetenda uhalifu wa kivita

Umoja wa Mataifa umesema pana dalili za wazi zinazoonyesha kwamba jeshi la Myanmar limetenda uhalifu wa kivita tangu kuangushwa kwa utawala wa kiraia nchni humo. Msemaji wa kitengo cha hali za binadamu, Ravina Shamdasani ameeleza kuwa Umoja wa Mataifa umeweza kubainisha mtindo wa uhalifu huo katika mwaka uliopita unaoonyesha kuwa uhalifu huo unapangwa na kuratibishwa na kwamba mfumo wa mashambulio unatekelezwa. Jeshi la Mynmar lilitwaa mamlaka mwaka uliopita na kuiondoa serikali ya Aung San Suu Kyi iliyochaguliwa kwa njia za kidemokrasia. Baada ya majeshi ya usalama kutumia mabavu dhidi ya watu waliokuwa wanafanya maandamano ya amani, maalfu ya wananchi wameunda vikosi vya wanamgambo ili kupambana na wanajeshi.

MATUKIO YA KISIASA
MATUKIO YA AFRIKA
MASUALA YA JAMII
MICHEZO
HABARI KWA LUGHA YA KIINGEREZA

Tazama vidio 03:36

Vidio zaidi

Mwaka mmoja wa Rais Samia madarakani

Mwaka mmoja wa Rais Samia madarakani

Zaidi ya wakimbizi milioni 2.8 wamekimbia vita Ukraine

Zaidi ya wakimbizi milioni 2.8 wamekimbia vita Ukraine

Je,mafuta yaliotumiwa muda murefu yanaathari kwa afya ?

Je,mafuta yaliotumiwa muda murefu yanaathari kwa afya ?

Je wafahamu kuhusu jamii ya Wabulushi nchini Kenya?

Je wafahamu kuhusu jamii ya Wabulushi nchini Kenya?

DW Kisuaheli Msichana Jasiri

Ulemavu sio kikwazo

Matangazo
TUFUATILIE KATIKA MITANDAO YETU YA KIJAMII