Wanajeshi wa Kijerumani watapelekwa Ufaransa
11 Februari 2009Hiyo ilitangazwa na Kansela wa Ujerumani Angela Merkel na Rais wa Ufaransa Nicolas Sarkozy katika mkutano wa usalama uliofanywa juma lililopita mjini Munich.Hatua ya kupeleka kikosi cha Ujerumani nchini Ufaransa inatazamwa kama ni tukio la kihistoria linaloshuhudiwa pia na wakongwe wa vita wa Ufaransa.
Mkongwe wa vita Robert Seggie alie na miaka 79 anazidi kupata shida kutembea lakini bado hutembelea shule katika jimbo la Elsass kueleza vipi Ufaransa ilivyokombolewa wakati wa Vita Vikuu vya Pili.Anasema,vita vya Elsass vilikuwa vigumu kama vile vya Normandy.Seguier kama mwanamaji, alishuhudia vita vya kuukomboa mji wa Strasbourg na umwagaji damu uliotokea darajani Germersheim kwenye mto Rhein.Na sasa kwenye televisheni ameona vipi Kansela Merkel na Rais Sarkozy wakitamka yale ambayo kwa miaka mingi wala hayakudhaniwa kuweza kutokea.Kansela Merkel alisema:
"Ni heshima na furaha kwetu,kwamba Ufaransa kwa mara ya kwanza tangu Vita Vikuu vya Pili inasema,kikosi cha pamoja cha Ujerumani na Ufaransa kiwe na kituo nchini Ufaransa pia"
Na Rais wa Ufaransa Nicolas Sarkozy akaongezea:
"Ni heshima pia kwamba sasa wanajeshi wa Ujerumani wanaweza kuwekwa daima katika ardhi ya Ufaransa.
Kama wanajeshi 600 au 700 wa Ujerumani kutoka kikosi cha pamoja cha Ujerumani na Ufaransa wanatazamiwa kuhamishwa kutoka kituo chao cha Müllheim kusini mwa Ujerumani na kupelekwa Illkirch karibu na mji wa Strassbourg. Kwa sasa,wanajeshi wa kikosi cha pamoja cha mataifa hayo mawili wana vituo vyao katika miji mitatu ya Kijerumani tu yaani Müllheim, Donaueschingen na Immendingen.Kikosi hicho kiliundwa mwaka 1989 kama sehemu ya sera ya pamoja ya Ulaya ya ulinzi.
Lakini urafiki wa Ujerumani na Ufaransa haukwenda umbali wa kuweza kuvumilia kuona wanajeshi wa Kijerumani katika ardhi ya Ufaransa.Kwani miaka ya uvamizi wa Ujerumani hukumbukwa kwa uchungu mkubwa.Sasa miaka mingi imepita na hali imebadilika.Hata wakongwe wa vita wenye usemi mkubwa wanaweza kuishi na kuistahmili hali hiiyo mpya.