Wakaazi wa Bani Walid waombwa kuuhama mji
13 Septemba 2011Wapiganaji hao wanajitahadharisha kutolitenga kabila la Warfalla, ambalo ni kubwa kabisa nchini Libya, kwa hivyo, wanajaribu kujizuia kupambana na watu hao, kabla ya kuchukuliwa hatua za kijeshi ili kuudhibiti mji huo ulio mojawapo ya ngome za mwisho za Kanali Muammar Gaddafi.
Viongozi wepya wa Libya wanataka kuudhibiti mji wa Bani Walid upesi iwezekanavyo, lakini wanasita kutumia mabavu pakiwepo hatari ya kusababisha mtengano wa kabila la Warfalla. Kufanya hivyo kutahatarisha jitahada zao za kutaka kuunda serikali inayoyajumuisha makabila yote. Wito uliotangazwa kwa njia ya redio kutoka mji wa jirani Tarhouna, umewaomba wakaazi wa Bani Walid kukimbilia maeneo yenye usalama. Mpiganaji mmoja, Abumuslim Abdu amesema, wamepewa amri na makamanda wao kuwa waangalifu na kuepusha maafa ya kiraia.
Wafuasi wa Gaddafi watoa changamoto kali
Pamoja na Sirte alikozaliwa Gaddafi na mji wa jangwani Sabha, Bani Walid ni ngome mojawapo ya mwisho ya Kanali Gaddafi. Wafausi wa kiongozi huyo alie mbioni,wametoa changamoto kali kuliko vile ilivyotarajiwa, wakishambulia kwa makombora na mizinga kutoka mji wa Bani Walid.Wapiganaji wa Baraza la Kitaifa la Mpito -NTC- na wakaazi wa Bani Walid wanasema, vikosi vya Gaddafi viliopo katikati ya mji huo,vingali vikiungwa mkono na wenyeji wengi wanaothubutu pia kupeperusha bendera za Gaddafi juu ya mapaa ya nyumba zao.
Hata hivyo,wapiganaji wa NTC wanatathmini kuwa takriban asilimia hamsini ya familia zilizokuwa zikiishi Bani Walid,zimekimbilia mji mkuu Tripoli ulio kaskazini mwa nchi na mji wa pwani wa Misrata, lakini wafuasi wengi wa Gaddafi wamebaki Bani Walid. Upinzani mkubwa kutoka mji huo umewashangaza hata wapiganaji wenyeji. Lakini wakaazi wanasema, kabila la Warfalla lina hofu kuwa watalipiziwa kisasi kwa sababu ya uhusiano wao wa karibu wa kimila na kabila la Gaddafi.
Nadharia kali hazitovumiliwa
Jitahada za kuirejesha hali ya kawaida zikiendelea nchini humo, mwenyekiti wa NTC, Mustafa Abdel Jalil hapo jana alisema, wanajaribu kuwa na taifa lenye utawala wa kisheria na ambako msingi wake ni sheria za Kiislamu. Akaongezea kuwa nadharia kali za mrengo wa kulia wala wa kushoto hazitovumiliwa.
Wakati huo huo, Rais wa Afrika Jacob Zuma hii leo amesema, Umoja wa Afrika kama shirika, haliwatambui viongozi wepya wa Libya. Jopo la Umoja wa Afrika kuhusu Libya, linalojumuisha viongozi wa Uganda, Mauritania, Mali na Congo-Brazaville litakutana hiyo kesho mjini Pretoria kujadili matokeo mapya ya nchini Libya.
Mwandishi: Martin,Prema/rter,afpe
Mhariri:Abdul-Rahman