1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

OPEC yapunguza ugavi huku kukiwa na hofu ya mfumuko wa bei

10 Oktoba 2022

Nchi zinazosafirisha mafuta kwa wingi duniani OPEC zilitangaza mnamo mwaka 2020 hatua ya kupunguza kwa kiasi kikubwa usambazaji wake duniani huku kukiwa na wasiwasi juu ya ongezeko la mfumuko wa bei.

https://p.dw.com/p/4I03P
Organization of the Petroleum Exporting Countries (OPEC)
Picha: RYAD KRAMDI/AFP/Getty Images

Hatua hiyo imeongeza mpasuko wa kidiplomasia kati ya kundi linaloungwa mkono na Saudi Arabia na lile la mataifa ya Magharibi, ambayo yana wasiwasi juu ya bei ya nishati ambayo itaathiri uchumi wa kimataifa ambao tayari ni dhaifu na pia kukwamisha juhudi za kuikosesha Urus mapato ya mafuta kufuatia uvamizi wake nchini Ukraine.

Mikataba ya ulimwengu ilifikiwa wiki hii baada ya Shirika la Nchi zinazosafirisha zaidi mafuta duniani na washirika wao, ikiwemo Urusi, kukubaliana siku ya Jumatano (05.10.2022) kupunguza uzalishaji wao kwa takriban mapipa milioni 2 kwa siku kabla ya msimu wa baridi kuanza.

Soma zaidi:OPEC+ wakubaliana kushusha kiwango cha uzalishaji mafuta

Washiriki wa sekta hiyo wamesema, hatua hiyo inaweza kusababisha ongezeko la bei ya juu zaidi, haswa kwa mafuta ya Mashariki ya Kati, ambayo yanakidhi karibu theluthi mbili ya mahitaji ya bara la Asia, na pia kuongeza wasiwasi wa mfumuko wa bei wakati serikali za Japan na India zinakabiliana na kupanda kwa gharama za maisha huku bara la Ulaya likitarajiwa katika majira ya baridi, kutumia zaidi nishati ya mafuta badala ya gesi ya Urusi.

Msemaji wa kampuni ya SK Energy ambao ni wasafirishaji wakubwa wa mafuta nchini Korea Kusini ameliambia Shirika la habari la Reuters kuwa wana wasiwasi juu ya kuibuka tena kwa bei ya mafuta ya kimataifa.

Soma zaidi: Mafuta yapanda bei baada ya mkutano wa OPEC kuvunjika

Korea Kusini, taifa la nne lenye uchumi mkubwa barani Asia na kitovu cha viwanda, imeshuhudia ongezeko la gharama za uzalishaji kutokana na kupanda kwa bei za bidhaa.

Bei ya pipa moja la mafuta ambayo huzingatiwa barani Ulaya (Brent) ilifikia dola 139.13 kwa pipa mwezi Machi, ikiwa ni kiwango cha juu zaidi tangu mwaka 2008, na hii ikiwa ni baada ya vita vya Ukraine kuzusha hofu ya kukosekana kwa usambazaji wa mafuta kutoka Urusi.

Makato halisi

Saudi Arabien | Öl-Lager am Hafen von Jubail
Kiwanda cha mafuta cha Jubail, Kaskazini Magharibi mwa Saudi ArabiaPicha: Bilal Qablan/AFP/Getty Images

Waziri wa Nishati wa Saudia Abdulaziz bin Salman amesema kwa uhalisia kiwango kinachotarajiwa kupunguzwa katika  usambazaji kinaweza kuwa kati ya pipa milioni 1 hadi 1.1 ili kukabiliana na kupanda kwa viwango vya riba duniani na uchumi wa ulimwengu unaodhoofika.

Hatua hiyo iliibua majibu makali kutoka Washington, ambayo ilikosoa mpango wa OPEC na kuutaja kama wenye mtazamo mfinyu. Ikulu ya Marekani ilisema kuwa Rais Joe Biden ataendelea kutathmini iwapo ataachilia zaidi hisa za kimkakati za mafuta ili kupunguza bei.

Tilak Doshi, Mkurugenzi mtendaji wa kampuni ya Doshi Consulting, ambaye hapo awali alikuwa ameajiriwa na Kampuni ya Saudi Aramco, anasmea Falme za Kiarabu (UAE) na Kuwait zina uwezekano wa kuchukua sehemu kubwa ya kupunguzwa kwa uzalishaji huo, na kwamba hilo ni pigo la OPEC kwa Biden na kuongeza kuwa uhusiano kati ya Urusi na Saudia unaonekana kuimarika zaidi.

Soma zaidi: UAE yapinga pendekezo la uchimbaji mafuta la OPEC

OPEC+ inapunguza wasiwasi wa usambazaji huku vikwazo vya Jumuiya ya Ulaya kwa mafuta ya Urusi vikiwa vilianza kutekelezwa Desemba na Februari mwaka huu.

Washiriki wa sekta hiyo wanakadiria hasara Urusi kufikia kati ya ujazo wa milioni 1 hadi 2 kwa siku, kulingana na jinsi Moscow inavyokabiliana na

bei ya mataifa ya G7 kwa mafuta ya Urusi.

Sera hiyo inalenga kuhakikisha mafuta ya Urusi yanaendelea kutiririka kwa nchi zinazoendelea kiuchumi lakini kwa bei ya chini ili kupunguza mapato ya Moscow.