1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani, washirika wazidisha mbinyo wa kiuchumi kwa Urusi

Iddi Ssessanga
12 Machi 2022

Marekani na washirika wake wameamua Ijumaa kusitisha uhusiano wa kawaida wa kibiashara na Urusi, huku Rais Joe Biden akiapa kuwa nchi za Magharibi zitamfanya Vladimir Putin alipe gharama ya uvamizi wake nchini Ukraine.

https://p.dw.com/p/48OAT
Präsident Biden zur Lage in der Ukraine
Picha: Al Drago/UPI/imago images

Biden alitangaza hatua hiyo mpya, ambayo itawezesha mataifa ya Magharibi kuweka viwango vya juu vya ushuru kwa bidhaa za Urusi, kwa uratibu na washirika wa NATO, Kundi la mataifa ya G7 na Umoja wa Ulaya.

Washington na Brussels pia zimesema kuwa zitakataza mauzo ya bidhaa za anasa kwa Urusi katika kile ambacho rais wa halamashauri kuu ya Umoja wa Ulaya Ursula von der Leyen amekielezea kama "pigo la moja kwa moja kwa matajiri wa Urusi."

"Marekani na washirika wetu na washirika wanaendelea kufungwa ili kuongeza shinikizo la kiuchumi kwa Putin na kuitenga zaidi Urusi katika hatua ya kimataifa," Biden alisema.

Putin "hawezi kuendeleza vita vinavyotishia msingi wa amani na utulivu wa kimataifa na kisha kuomba msaada kutoka kwa jumuiya ya kimataifa."

Soma pia: EU yaungana kuhusu Ukraine, lakini haitatoa uanachama wa haraka

Ikiwa ni kanuni muhimu ya Shirika la Biashara Ulimwenguni, kile kinachojulikana kama hadhi ya taifa linalopendelewa zaidi, maarufu nchini Marekani kama mahusiano ya kawaida ya kudumu ya biashara (PNTR), inahitaji nchi kudhaminiana ushuru sawa na utendeanaji wa kisheria.

Biden alionya katika hotuba yake katika Ikulu ya White House kwamba "Putin lazima alipe gharama" kama "mchokozi" katika vita dhidi ya jirani yake.

Ukraine-Konflikt - USA Präsident Joe Biden
RAis Joe Biden akiwa katika mkutano wa vidio na rais wa Ufaransa Emmanuel Macron, kansela wa Ujerumani Olaf Scholz na waziri mkuu wa Uingereza Boris Johnson wakijadili mzozo wa Ukraine.Picha: Adam Schultz/The White House/AP/dpa/picture alliance

Wabunge wa Marekani -- ambao ndiyo watakuwa na uamuzi wa mwisho -- tayari wameonyesha kuunga mkono Urusi kupokonywa hadhi ya upendeleo ambayo inahakikisha kutendewa sawa kati ya washirika wa biashara wa kimataifa.

Katika taarifa iliyotolewa mjini Berlin, viongozi wa G7 walithibitisha kwamba kila mmoja "atajitahidi" kuchukua hatua ya kunyima Urusi hadhi ya upendeleo wa kibiashara. 

Kuiondolea Moscow hadhi hiyo, iliyopatiwa Desemba 2012, kutamruhusu Biden kuzitoza ushuru mkubwa bidhaa za Urusi au kuzuia uagizaji wake.

Soma pia: Mataifa ya Magharibi yaendelea kuisaka suluhu mzozo Ukraine

Hatua hiyo haitakuwa na athari ya haraka kwa uchumi wa Urusi, lakini pamoja na vikwazo vingine ambavyo Marekani na washirika wake wameiwekea, wazo ni kuongeza mbinyo kwa rais Vladmir Putin na kumlaazimisha kurudisha nyuma majeshi yake kutoka Ukraine.

Rais Biden pia alitangaza kupiga marufuku uagizaji wa vodka ya Urusi, almasi na vyakula vya baharini nchini Marekani.

Baadaye siku hiyo, wizara ya fedha ya Marekani ilitangaza safu ya vikwazo vipya vinavyolenga "wasomi na watendaji wa sekta ya biashara ambao ni washirika na wawezeshaji wa serikali ya Urusi."

Hawa ni pamoja na wanafamilia wa msemaji wa Putin, wajumbe wa bodi ya benki iliyowekewa vikwazo ya VTB na wajumbe 12 wa baraza la chini la bunge la Urusi. 

Vikwazo vya hivi vya karibunini zaidi ni vinahitimisha duru kadhaa za vikwazo vya kibiashara vinavyokusudiwa kukata uhusiano wa kiuchumi na kifedha wa Russia na mataifa mengine duniani kutokana na uvamizi wake nchini Ukraine.

Soma pia: Zelensky: Watu 100,000 waondolewa miji ya Ukraine

Vimejumuisha kupiga marufuku uagizaji wa mafuta kutoka Urusi, kukamata mali za mabilionea wanaohusishwa na Putin, na kufungia akiba ya taifa ya pesa taslimu.

Ukraine-Konflikt - Russlands Präsident Wladimir Putin
Rais wa Urusi Vladmir PutinPicha: Mikhail Klimentyev/Sputnik Kremlin/AP/dpa/picture alliance

Kwa pamoja, hatua hizo tayari zimeisukuma Moscow kwenye ukingo wa kutolipa deni. Hatua hizo pia zimesababisha bei za bidhaa muhimu, kama vile petroli na ngano, kupanda, na kuwaumiza watumiaji wa Marekani ambao tayari wanakabiliwa na mfumuko wa bei wa juu zaidi katika miongo minne.

Wataalamu wa biashara hata hivyo wana shaka kuhusu kama ushuru mpya utakuwa na ufanisi.

"Biashara ya moja kwa moja ya Marekani na Urusi ni ndogo, kwa hivyo ushuru wa juu haungefanya uharibifu mkubwa kwao lakini unaweza kuongeza gharama kwa watengenezaji wetu ambao wanazitegemea kwa malighafi muhimu," William Reinsch wa Kituo cha Mafunzo ya Kimkakati na Kimataifa mjini Washington alisema.

Marekani yaishutumu Urusi kwa kutumia baraza la Umoja wa Mataifa kupotosha

Marekani iliishutumu Urusi kwa kutumia mkutano wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa Ijumaa "kudanganya na kueneza habari za upotoshaji" kama sehemu ya uwezekano wa operesheni ya uongo ya Moscow ili kutumia kemikali au silaha za kibayolojia nchini Ukraine.

Soma pia:Urusi inahujumu makubaliano ya Nyuklia ya Iran ?

Balozi wa Marekani Thomas-Greenfield alisema Urusi ilikuwa ikicheza kile kilichoelezwa katika baraza hilo mwezi uliopita na waziri wa mambo ya nje wa Marekani Antony Blinken _ kwamba Rais Vladimir Putin "atatengeneza madai kuhusu silaha za kemikali au za kibayolojia ili kuhalalisha mashambulizi yake ya kikatili dhidi ya watu wa Ukraine. ''

"Nia ya uongo huu inaonekana wazi, na inatia wasiwasi sana,'' alisema. "Tunaamini kuwa Urusi inaweza kutumia kemikali au sumu ya kibayolojia kufanya mauaji, kama sehemu ya tukio la uwongo, au kusaidia operesheni za kimbinu za kijeshi.''

Marekani imeonya kuhusu operesheni hizo za Urusi sambamba na uvamizi ulioanza Februari 24. Urusi ilikuwa imeomba mkutano huo kushughulikia madai yake ya "shughuli za kibayolojia'' za Marekani nchini Ukraine, madai yaliyotolewa bila ushahidi wowote na kukanushwa na Washington na Kyiv.

Balozi wa Russia katika Umoja wa Mataifa Vassily Nebenzia alisema Wizara yake ya Ulinzi ina nyaraka zinazodai kwamba Ukraine ina angalau maabara 30 za kibaolojia zinazofanya "majaribio hatari sana ya kibiolojia'' yanayohusisha vimelea vya magonjwa, na kazi yake "inafanywa na kufadhiliwa na kusimamiwa na idara ya Kupunguza Tishio la Ulinzi ya Marekani."

Soma zaidi:Urusi,Ukraine washindwa kufikia mwafaka huko Uturuki

Ukraine ina mtandao wa maabara za kibaolojia ambazo zimepata ufadhili na usaidizi wa utafiti kutoka Marekani, lakini zinamilikiwa na zinaendeshwa na Ukraine na ni sehemu ya mpango unaoitwa Mpango wa Kupunguza Vitisho vya Kibiolojia ambao unalenga kupunguza uwezekano wa milipuko hatari, iwe ya asili au ya kibinadamu. Juhudi za Marekani zilianza kufanya kazi katika miaka ya 1990 ili kusambaratisha mpango wa zamani wa Umoja wa Kisovieti wa silaha za maangamizi makubwa. 

"Maabara hizo sio za siri,'' alisema Filippa Lentzos, mhadhiri mkuu wa sayansi na usalama wa kimataifa katika Chuo cha King's College London, katika barua pepe kwa shirika la habari la Associated Press. "Hazitumiwi kuhusiana na silaha za kibayolojia. Haya yote ni upotoshaji.''

Balozi wa Uingereza wa Umoja wa Mataifa Barbara Woodward, aliyaita madai hayo "upuuzi mtupu'' na kusema "Urusi inazama kwa kina kirefu leo, lakini baraza hilo halipaswi kuburuzwa nalo.''

Soma pia: Mawaziri wa mambo ya nje Urusi na Ukraine wakutana Uturuki

Mkuu wa kupunguza matumizi ya silaha wa Umoja wa Mataifa Izumi Nakamitsu aliliambia baraza hilo kuwa anafahamu juu ya ripoti za vyombo vya habari kuhusu madai hayo na akasema: "Umoja wa Mataifa haufahamu mipango yoyote ya silaha za kibiolojia.''

Balozi wa China katika Umoja wa Mataifa Zhang Jun alionyesha wasiwasi kuhusu shutuma za Russia na akahimiza uchunguzi "kutoa ufafanuzi wa kina na kukubali uthibitisho wa pande nyingi.''

Raia wa Ukraine wazidi kukimbia nchi

Balozi wa Ukraine katika UN, Sergiy Kyslytsya alisema shutuma za Moscow "huenda kweli zinaelekeza kwa Urusi kuandaa operesheni nyingine ya kutisha ya kuandaa matukio ya uongo.''

Akibainisha kuwa Urusi tayari imetumia makombora ya kasi, kurusha roketi nyingi na mashambulizi makubwa ya angani, balozi Kyslytsya alimwambia Putin kwa kuuliza: "Kwa hiyo ni nini kingine utakachotumia dhidi ya Ukraine?''

Soma pia: Urusi yashambulia hospitali tatu Ukraine

Ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa, wakati huo huo, imepokea "ripoti za kuaminika'' kwamba vikosi vya Urusi vinatumia mabomu ya mtawanyiko nchini Ukraine, ikiwa ni pamoja na katika maeneo yenye watu wengi ambayo yalipigwa marufuku chini ya sheria ya kimataifa ya kibinadamu, Naibu Katibu Mkuu Rosemary DiCarlo aliliambia Baraza la Usalama.

Urusi yaibana Kyiv huku janga 'lisilofikirika' likikaribia Ukraine

Vikosi vya Urusi vilielekea Kyiv na kushambulia maeneo ya raia katika miji mingine ya Ukraine Ijumaa, na kusababisha maonyo juu ya uwezekano wa janga.

Siku 16 baada ya Moscow kuushangaza ulimwengu kwa kuivamia Ukraine, Umoja wa Mataifa na mataifa mengine yalisema huenda inatekeleza uhalifu wa kivita katika miji kama Mariupol, ambao kwa siku kadhaa sasa umezingirwa na vikosi vya Vladimir Putin.

Maafisa katika mji huo wa bandari wa kusini, wamesema jana kwamba watu zaidi ya 1,500 wameuawa wakati wa mzingiro wa Urusi uliodumu kwa siku 12.

Soma piaWaukraine wakimbia huku marufuku ya mafuta ya Marekani ikikaribia

Walionusurika wamekuwa wakijaribu kukimbia mashambulizi ya Urusi katika mji wa baridi ulioachwa bila maji au joto, na kukosa chakula. Hali ni "ya kukata tamaa," afisa wa shirika la Madaktari Wasio na Mipaka alisema.

"Mamia kwa maelfu ya watu... wamezingirwa kwa nia na madhumuni yote," Stephen Cornish, mmoja wa wale wanaoongoza operesheni ya shirika hilo la kitabibu nchini Ukraine, aliiambia AFP katika mahojiano.

Raia wa Ukraine waliopo Tanzania wauzungumzia mzozo wa nyumbani kwao.

"Mizingiro ni mabo ya zama za kati ambayo imeharamishwa na sheria za kisasa za vita kwa sababu nzuri."

Wakati Urusi ikitanua mashambulizi yake na mazungumzo kati ya Moscow na Kyiv yakionekana kutokwenda popote, maombi ya rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky ya kutaka NATO kuingilia kati yamekua ya kukata tamaa.

Rais Joe Biden, jana Ijumaa aliondoa uwezekano wa hatua za moja kwa moja dhidi ya Urusi yenye silaha za nyuklia, akionya kwamba hilo linaweza kusababisha "Vita Kuu ya Tatu ya Dunia."

Soma pia: ''Sisi ni taifa ambalo lilivunja mipango ya adui'' Zelensky

Badala yake Washington iliongeza vikwazo zaidi juu ya vile ambavyo tayari vinadhoofisha uchumi wa Urusi, safari hii ikisitisha uhusiano wa kawaida wa kibiashara na kutangaza kupiga marufuku bidhaa maarufu za Kirusi za vodka, vyakula baharini na madini ya almasi.

Marekani na Umoja wa Ulaya pia zilisitisha uuzaji wa bidhaa zao za anasa kwa Urusi.

"Putin lazima alipe gharama. Hawezi kuendeleza vita vinavyotishia msingi wa amani na utulivu wa kimataifa na kisha kuomba msaada kutoka kwa jumuiya ya kimataifa," Biden alisema kutoka Ikulu ya Marekani.

Alizungumza huku Umoja wa Mataifa ukisema watu milioni 2.5 sasa wamekimbia Ukraine na karibu milioni mbili wamelazimika kuyahama makazi yao kutokana na vita hivyo.

Chanzo: Mashirika