1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Huduma maalum kwa wanafunzi wa kigeni

Maja Dreyer30 Novemba 2006

Vijana laki mbili hivi kutoka kila pembe ya dunia wanasoma kwenye vyuo vikuu hapa nchini Ujerumani. Lakini si wote kati wao wanaoweza kumaliza masomo yao, kati ya wanafunzi 10 wa kigeni, watano au sita wanaacha masomo yao bila ya kupata digrii. Kwa sababu hiyo, vyuo vingi vinaanzisha huduma maalum kwa wanafunzi wa kigeni, ila tu taratibu zao zinatofautiana.

https://p.dw.com/p/CHm4
Kwenye chuo kikuu cha Leipzig
Kwenye chuo kikuu cha LeipzigPicha: dpa

Ni mwaka huu tu, serikali ya Ujerumani imeamua, wanafunzi wa kigeni wanaosoma kwenya chuo kikuu hapa nchini, wataruhusiwa kuongeza muda wao wa kukaa Ujerumani ili kutafuta kazi.

Kwa sababu hiyo ilibidi vyuo vikuu pia vibadilishe huduma zao kwa wanafunzi hao wa kigeni, kama Birgit Roser wa taasisi ya Kijerumani ya kubadilishana wanafunzi na wasomi anavyoeleza: “Kimsingi nia yetu sio tena kuwasomesha tu wanafunzi hawa na halafu kuwarudisha nyumbani, bali pia kuwaunganisha vijana wa kigeni wenye vipaji vikubwa katika jamii ya Ujerumani. Tunataka vyuo vyetu vipate faida kutokana na wanafunzi wa kigeni, lakini pia wawe ni raia na wafanya kazi wa Ujerumani.”

Idara zinazoshughulikia masuala ya wanafunzi wa kigeni zinakubali kwamba wanafunzi hawa wanahitaji huduma maalum, lakini tena lazima huduma hizo zilipwe. Kwa sababu hiyo, wanafunzi wa chuo kikuu cha mji huu wa Bonn wanaotoka nchi zisizo wanachama wa Umoja wa Ulaya wanalazimishwa kulipa Euro 150 kwa muhula kwa huduma hizo. Yale wanayopata ni kozi maalum za lugha na vipi kuratibu masomo yao.

Kwa wanafunzi lakini, malipo haya ni mzigo mwingine. Sylvia Raitschewska anatoka Bulgaria ambayo bado haijawa mwanachama wa Umoja wa Ulaya. Amesoma Bonn kwa miaka mitatu sasa. Alipoanza, masomo yalikuwa bure. Lakini sasa analipa kiasi Euro 650 kila muhula kwa masomo na huduma maalum kwa wanafunzi wa kigeni.

Kulipa hayo yote ni vigumu kwake, anasema Sylvia: “Naishi katika dunia mbili, yaani chuoni na kazini. Kuna wakati ambapo nafanya kazi kuliko kwenda chuoni. Halafu sifahamu kwa nini mimi nahitaji huduma hizo, na wanafunzi wa Uhispania, Ufaransa na kwengineko hawalazimiki kuzichukua. Kwangu mimi ni wazi kwamba: Wajerumani hawataka sisi kuja hapa. Labda pia wanafunzi wa kigeni kama sisi hatuna nguvu za kisheria.”

Jumuiya ya wanafunzi wa Bonn pia inapinga karo hizo za huduma kwa wanafunzi wa kigeni. Kwa kweli, vyuo vikuu vingine vya Ujerumani vinatoa huduma hizo maalum bila ya kuongeza malipo. Wale wanaowahudumia wanafunzi wapya wa kigeni, wenyewe wanatoka nchi za kigeni, lakini wameishi Ujerumani kwa muda. Kwa hivyo, ikiwa wanafunzi wa kigeni wanakuja Ujerumani, shauri moja ni kuangalia wapi watakapolipishwa kwa huduma watakazozipata.