Ujerumani kumchagua rais mwanamke kumrithi Steinmeier?
5 Machi 2026
Rais wa sasa nchini Ujerumani ni Frank Walter Steinmeier ambaye muhula wake wa pili madarakani unamalizika mwanzoni mwa mwaka ujao, 2027. Chama cha siasa za wastani za mrengo wa kushoto cha Social Democratic SPD na wanamazingira wanapigia upatu mara hii nafasi hiyo irithiwe na mwanamke.
Hatua hiyo itakuwa ni ya kihistoria hasa ikizingatiwa Ujerumani imekuwa na marais 12 wote wanaume tangu kumalizika vita vya pili vya dunia. Jina la kansela wa zamani Angela Merkellilipotajwa kuwa miongoni mwa wanapaswa kurithi nafasi hiyo, mjadala mkubwa umezuka,suala hilo likigonga vichwa vya habari. Chama cha kijani kimependekeza jina la Kansela huyo wa zamani kugombea.
Merkel aliiongoza Ujerumani kwa miaka 16 mpaka mwaka 2021 na alikuwa kiongozi aliyepata umaarufu mkubwa katika kipindi chote cha utawala wake. Hata hivyo Merkel amepuuza mara moja atiati zinazosambaa kuhusu kumrithi Steinmeir akiziita tetesi hiyo kuwa hazina maana.
Wanaofuatilia masuala ya kisiasa wanasema kwamba pendekezo hilo huenda pia lisifanikiwe kwasababu ya uhasama wa muda mrefu kati ya Merkel na kansela wa sasa Friedrich Merz.
Hivi karibuni Merz alikiambia kituo cha Televisheni cha Phoenix kwamba pendekezo lake kuhusu nani arithi kiti cha rais Steinmeir atalitangaza mwezi Septemba.
Kiongozi huyo wa Ujerumani kutokana chama cha CDU amesema anataka kumchagua mtu atakayekuwa mwakilishi wa nchi kwa ujumla wake, lakini hakutaja ikiwa mtu anayemfikiria ni mwanamke au mwanamme.
Ikumbukwe kwamba chaguzi za mwisho mwaka huu za majimbo matano zitafanyika mwezi Septemba na hapo ndipo itakapobainika mwelekeo hasa wa kisiasa kitaifa.
Kimsingi rais wa Ujerumani hachaguliwi na wananchi moja kwa moja, baraza kuu la bunge ndilo linalowajibika kupiga kura ya siri kumchagua rais anayekaa kwa muhula wa miaka mitano na kisha kuchaguliwa tena kwa muhula wa pili wa mwisho.
Baraza hilo linajumuisha wabunge 630 wa mabaraza yote sambamba na wawakilishi wa majimbo yote 16 ya Ujerumani na wawakilishi hao wanaweza kuwa wanasiasa lakini pia hata raia wenye umaarufu kwenye jamii kama wanariadha au wasanii.