1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Serikali ya Ujerumani yakabiliwa na mwaka mgumu mbele yake

Sabine Kinkartz | Iddi Ssessanga
4 Januari 2024

Vyama vya serikali ya muungano ya Ujerumani, SPD, Kijani na FDP vimegawanyika zaidi kuliko kuungana, na hakutakuwa na pesa za kutosha kutatua tofauti hizo. Lakini 2024 unaweza kuwa umeanza vibaya hata zaidi kwa serikali.

https://p.dw.com/p/4aq2Y
Ujerumani| Makubaliano kuhusu bajeti ya 2024
Rober Habeck kutoka chana cha Kijani (kushoto), Kansela Olaf Scholz wa SPD (katikati), na Christian Lindner wa FDP (kulia) watapa ugumu kuendeleza muungano wao.Picha: Michael Kappeler/dpa/picture alliance

Hasira zimekuwa zikiongezeka katika chama cha FDP kwa miezi kadhaa sasa. Chama hicho mshirika mdogo kabisa kwenye serikali ya muungano ya shirikisho kimepata kipigo kimoja baada ya kingine katika chaguzi za majimbo na mitaa mnamo 2022 na 2023.

Wanasiasa wa ndani wamesema ushirikiano usio na furaha mjini Berlin ndio wa kulaumiwa. Kura za maoni zinaonyesha kuwa ni raia mmoja tu kati ya watano ambaye bado ameridhika na kazi ya vyama vya mrengo wa kushoto vya Social Democratic Party (SPD), Greens na FDP katika serikali ya shirikisho.

Wapo wengi ndani ya FDP wanaoamini kuwa njia ya kuondoka kwenye mkwamo huu ni kwa chama hicho kujitoa katika serikali ya mseto, ambayo wanadhani inakirudisha nyuma. Uchunguzi wa wanachama wa chama, ambao ulihitimishwa mnamo Januari 1, 2024, ulipaswa kusafisha njia kwa ajili ya hili. Hata hivyo, asimilia 52 ya wanachama wa chama cha FDP waliopiga kura walichagua kusalia katika muungano huo.

Kuwa watulivu na kuendelea?

Matokeo hayo huenda yalisababisha ahueni katika makao makuu ya vyama vitatu tawala. Ingawa kura hiyo haina nguvu kisheria, uongozi wa chama cha FDP haungeweza kupuuza wengi waliounga mkono kuondoka. Muungano wa serikali kuu unaojulikana  kama "Ampel" au taa za barabarani kutokana na rangi za vyama washirika, ungekuwa chini ya shinikizo zaidi.

Soma pia: Licha ya utajiri, Ujerumani yahsindwa kupunguza watu wasio na makazi

Baada ya kura kuhesabiwa, uongozi wa chama cha FDP ulikimbilia kupigia chapuo kura hiyo finyu ya kubaki kama mafanikio, ambapo Katibu Mkuu wake Bijan Djir-Sarai, akisema chama hicho kinataka kuwajibika kwa nchi na kuchangia maendeleo yake. "Wanachama wa chama wanataka kuona muhuri wa wazi wa kiliberali kwenye sera ya serikali. Matokeo yake yanaimarisha azimio letu la kukabiliana na changamoto kubwa zinazoikabili nchi," aliongeza.

Ujerumani | Kansela Olaf Scholz
Kansela Olaf Scholz alikiri katika hotuba yake ya mwana mpya kwamba raia wengi hawaridhiki na utendaji wa serikali yake.Picha: Markus Schreiber/AP/picture alliance

Umaarufu unaozidi kupungua

Kimsingi matokeo ya Jumatatu yataweza kutoa tu ahueni ya muda. Hiyo ni kwa sababu 2024 ni mwaka wa uchaguzi, na uchaguzi wa Ulaya utafanyika Juni 9 na mabunge ya majimbo ya Saxony, Thuringia na Brandenburg yatachaguliwa tena Septemba. Uchaguzi wa mitaa pia unatarajiwa kufanyika katika majimbo tisa kati ya 16 ya shirikisho.

Katika majimbo ya Saxony, Thuringia na Brandenburg, Chama Mbadala cha Ujerumani, AfD, ambacho kimeainishwa na Ofisi ya Ulinzi wa Katiba kuwa chenye siasa kali za mrengo wa kulia, ndicho chama chenye nguvu zaidi. Chama cha Christian Democratic Union pekee ndio kinaonesha nguvu. Vyama vya SPD, Kijani na FDP viko nyuma sana, vikiwa na uungwaji mkono wa tarakimu moja katika baadhi ya kura za maoni.

Vyama hivyo vitatu pia vimepoteza uungaji mkono mkubwa katika ngazi ya shirikisho tangu kuingia madarakani Desemba 2021. Wakati awali vilikuwa na wingi na jumla wa asilimia 52 ya kura, viwango vyao vya umaarufu katika kura za maoni sasa vimeshuka hadi asilimia 32.

Katika hotuba kwa taifa kwenye mkesha wa mwaka mpya, Kansela Olaf Scholz alikiri kuwa watu wengi hawajaridhika. "Ninazingatia hilo moyoni," alisema. Lakini ulimwengu umekuwa wa machafuko na mgumu zaidi na unabadilika "kwa kasi ya kushangaza," aliongeza, akisema Ujerumani lazima ibadilike pia.

Umaarufu wa Scholz waziri kuporomoka

Lakini je, ni kweli mabadiliko ndiyo watu wanahangaika nayo, au ni jinsi serikali ya mseto inavyokabiliana na migogoro mingi na matokeo yake? Hii ni pamoja na mzozo wa nishati uliofuatia vita vya Urusi nchini Ukraine, kupanda kwa bei na kudorora kwa uchumi wa Ujerumani.

Soma pia: Wakulima wa Ujerumani wauzingira mji Berlin katika mgomo wa trekta

Pengine hata Kansela mwenyewe amebaini namna umaarufu wake ulivyoshuka katika uchunguzi wa maoni, hii ikisababishwa hasa na mtindo wake wa mawasiliano.

Berlin | Mwenyekiti wa FDP Christian Lindner
Mwenyekiti wa chama cha FDP na waziri wa fedha wa Ujeurmani, Christian Lindner. Picha: Annegret Hils/REUTERS

Mara nyingi vyama vya muungano vinapolumbana, na hivyo ndivyo hali ilivyokuwa mara kwa mara mwaka 2023, Scholz anapenda kujiweka kando na macho ya umma, na kuzungumza pale tu anapoona ni muhimu kabisa.

Ujerumani yakabiliwa na pengo kubwa la bajeti

Pengine 2024 utakuwa mwaka mgumu zaidi wa muhula wa serikali ya muungano. Mbali na tofauti zote za kisiasa na kiitikadi, sasa pia kuna mzozo juu ya pesa.

Muungano huo ni ushirika wa chama kimoja cha nadharia za uchumi wa kiliberali na viwili vya mrengo wa kushoto. SPD na Greens wanasimia hali thabiti na wanataka pesa nyingi kwa ajili ya ustawi wa jamii na ulinzi wa tabianchi. FDP ina maoni tofauti, ikisisitiza juu ya uwajibikaji wa mtu binafsi na matumizi kidogo ya serikali.

Ili kusawazisha mizozo hii, Scholz, ambaye bado alikuwa waziri wa fedha wa shirikisho mnamo 2021, alikuja na mbinu ya ujanja. Alipendekeza kwamba uidhinishaji wa mkopo ambao haujatumika wa euro bilioni 65, ambazo bunge liliidhinisha mnamo 2021 wakati wa janga la COVID-19, zihamishiwe katika hazina maalum chini ya serikali yake.

Soma pia: Waziri wa nje wa Ujerumani ajitenga na wazo la kuhamishia waomba hifahi Rwanda

Bajeti iliyopendekezwa ilitoa fedha za kutosha kwa ajili ya mipango ya kisiasa ya SPD na Kijani, wakati huo huo ikimwezesha waziri wa fedha wa FDP, Christian Lindner, kutoa bajeti ya shirikisho ya kawaida bila kuchukua deni lolote jipya.

Mpango huo ulifanya kazi kwa chini ya miaka miwili tu. Kisha mwezi Novemba 2023, Mahakama ya Kikatiba ya Shirikisho iliamua kuwa ubadilishaji wa matumizi ya fedha za janga ulikuwa kinyume cha katiba. Kama matokeo ya uamuzi huo, bajeti ya serikali ya mseto haitoshi tena, na ukopaji zaidi unadhibitiwa sana na kanuni ya ukomo wa deni ya kikatiba ya Ujerumani, ambayo ilianzishwa mnamo 2009.

Serikali ya mseto sasa italazimika kuweka akiba kwa muda wake wote madarakani, lakini itakuwa angalau na nafasi ya kupumua. Mzozo kuhusu pesa unaweza kusababisha mifarakano zaidi katika miezi ijayo.

Ujerumani: Hatutaiacha Ukraine kwenye vita peke yake

Ni matumizi gani yalio muhimu?

Katika mkutano wa chama cha SPD, Scholz alisema Ujerumani inaweza kulazimika kutoa pesa zaidi kwa ajili ya Ukraine "ikiwa wengine watadhoofika" - ishara ya wazi kuhusu hali ya kisiasa nchini Marekani kabla ya uchaguzi wa rais wa 2024. Kwa hivyo, alisema, maamuzi yanahitajika kufanywa kwa upande wa Ujerumani ili kuhakikisha "kwamba [Ujerumani] iko katika nafasi ya kufanya hivyo."

Kansela huyo alikuwa anarejelea waziwazi sheria ya ukomo wa madeni ya  Ujerumani, ambayo inalazimu serikali ya shirikisho na serikali za majimbo kusawazisha mapato na matumizi yao. Scholz ameweza kumshawishi Waziri wa Fedha Lindner kwamba angalau watajadili kusitisha tena utekelezaji wa sheria ya madeni mwaka huu, ikiwa itabainika kuwa msaada wa kijeshi na kifedha kwa Ukraine unahitaji kuongezwa zaidi.

Soma pia: Baraza la mawaziri Ujerumani lakutana kukwamua mkwamo

Lakini hii haimaanishi kuwa FDP itakubali. Utafiti wa wanachama wa FDP ulionyesha kuwa asilimia 48 walitaka kuvunjwa kwa muungano, na idadi hiyo inaweza kukua kwa urahisi.

Viongozi wa chama wanaogopa mgawanyiko kuliko kitu kingine chochote. Katika tukio la uchaguzi mpya, hawatalazimika tu kuogopa kupoteza mamlaka, lakini wabunge wengi pengine pia wangelazimika kuacha viti vyao katika Bundestag.

Ndio maana katika ngazi ya viongozi na katika makundi ya wabunge, kila mtu anajaribu kuufanya muungano uendelee. Hofu ya kupoteza kisiasa ndiyo kitu pekee kitakachowaunganisha washirika wa muungano mwaka wa 2024.