1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

NATO yakiri mapungufu katika mbinu zake za kijeshi Libya

20 Aprili 2011

Wakati Jumuiya Kujihami ya NATO ikiendeleza mashambulizi ya anga dhidi ya vikosi vya kiongozi wa Libya, Kanali Muammar Gaddafi, jeshi la muungano limekiri kuwepo mapungufu katika mbinu zake za kijeshi.

https://p.dw.com/p/10wts
Mkuu wa vikosi vya NATO, Brigedia Jenerali Mark van UhmPicha: picture-alliance/dpa

Mkuu wa vikosiv ya muungano vya NATO, Brigedia Jenerali Mark van Uhm amekiri hayo kwa sababu ya hatari ya kutokea mauaji ya raia na kwamba wanalazimika kuzuia mashambulizi ya anga kwenye miji. Jenerali huyo amesema wanachukua kila tahadhari kuepuka kufanya mauaji kutokana na mashambulio yao ya anga.

Taarifa hiyo ya Jenerali Van Uhm ameitoa wakati vikosi vinavyomtii Kanali Gaddafi vikiendelea kuushambulia mji wa tatu kwa ukubwa wa Misrata ambao unadhibitiwa na waasi.

Abdel-Fattah Younis
Kiongozi wa jeshi la waasi wa Libya, Abdel-Fattah YounisPicha: AP

Baadhi ya mataifa wanachama wa NATO wamekuwa wakijadiliana njia ya kuwasaidia waasi bila kupeleka majeshi yao ya nchi kavu.

Marekani imesema imeweka wazi fursa ya kupeleka silaha kwa vikosi vya waasi, huku Italia ikiwa imekutana na viongozi wa waasi kujadili namna ya kuwezesha mafuta yanayotoka kwenye maeneo wanayoyadhibiti kuuzwa nje.

Uingereza imesema itapeleka kundi la maafisa kwenye mji wa Benghazi ambao ni ngome kuu ya waasi kuwapatia ushauri kuhusu mawasiliano na mipangilio mizuri.