Mamilioni ya Walibya wahitaji msaada wa kibinaadamu
18 Mei 2011Matangazo
Mratibu wa Misaada wa Umoja wa Mataifa nchini Libya, Panos Moumtzis, anasema watu wapatao 1,600,000 wanahitaji msaada kwa sababu mapigano yamevuruga huduma zote za msingi na kusababisha uhaba wa chakula na madawa.
Moumtzis anasema idadi hiyo ni pamoja na watu 460,000 walioyakimbia makaazi yao kwa sababu ya mapigano. Wengine 500,000 waliovuka mipaka kuingia Tunisia, Misri na kwengineko katika eneo hilo la Afrika Kaskazini, nao pia wanahitaji msaada.
Mjumbe huyo leo (18.05.2011) aliwaomba wafadhili wa kimataifa msaada wa dola milioni 408, kugharimia shughuli za misaada za Umoja wa Mataifa nchini Libya hadi kufikia mwezi Septemba mwaka huu.
Mwandishi: Mohammed Abdul-Rahman
Mhariri: Mohammed Khelef