KABUL: Watoto saba wauwawa kwenye shambulio la angani
18 Juni 2007Watoto saba na wanagambo saba waliuwawa kwenye shambulio la angani lililofanywa na jeshi la muungano linaloongozwa na Marekani nchini Afghanistan. Shambulio hilo lililenga shule ya kidini ya kundi la al-Qaeda mashariki mwa Afghanistan.
Katika taarifa yake jeshi la muungano limesema wanamgambo wawili walitiwa mbaroni kwenye operesheni hiyo.
Shambulio hilo dhidi ya uwanja uliokuwa na msikiti na madrasa lilifanywa jana kwenye mkoa wa Paktika.
Sambamba na hayo, maafisa wa usalama wanaochunguza shambulio la bomu dhidi ya basi la polisi mjini Kabul wamemkamata mwanamume mmoja mwenye mafungamano na kundi la Taliban ambaye inadaiwa alipiga picha ya video mlipuko huo wakati ulipotokea.
Watu 35 waliuwawa kwenye shambulio hilo la jana ambalo limeelezwa kuwa baya zaidi kuwahi kufanywa na wanamgambo wa Taliban nchini Afghanistan.