1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Czech yachukuwa hatamu za uongozi wa Umoja wa Ulaya kutoka Ufaransa

Mohamed Dahman30 Desemba 2008

Jamhuri ya Czech inachukuwa hatamu za urais wa kupokezana wa Umoja wa Ulaya kutoka Ufaransa Alhamisi ikikabiliwa na masuala mbali mbali makuu ikiwa ni pamoja na mzozo unaozidi kuwa mkubwa wa usambazaji wa gesi na Urusi.

https://p.dw.com/p/GP7F
Rais wa Czech Vaclav Klaus (kushoto) na Waziri Mkuu wake Mirek Topolanek.Picha: picture-alliance/ dpa

Jamhuri ya Czech inasema haina maana kujiwekea malengo makubwa mno wakati ikishika uongozi ambapo itayapa kipau mbele mambo matatu usalama wa nishati, uhusiano wa nje na uchumi wakati wa kipindi cha mgogoro.

Naibu Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Czech Alexandr Vondra amesema kufuatia miezi kdhaa ya maandalizi nchi hiyo ya kikomunisti ya zamani ambayo imejiunga na Umoja wa Ulaya hapo mwaka 2004 iko tayari kwa mtihani wake wa uvumilivu wa miezi sita.

Katika kipindi cha wiki zilizopita maafisa wa serikali ya Czech wamekuwa wakipambana na wasi wasi juu ya uwezo wa kuchukuwa hatamu za Umoja wa Ulaya kutoka Ufaransa huku kukiwa na mgogoro wa kiuchumi duniani na baada ya kipindi cha mafanikio cha Ufaransa kilichohodhiwa na Rais Nicolas Sarkozy.

Dhima ya Waziri Mkuu wa Czech Mirek Topolanek kama rais wa Umoja wa Ulaya madarakani itakuwa ngumu zaidi kutokana na Rais Vaclav Klaus wa Czech kutowekea matumaini umoja huo na kuendelea kukosoa mambo mengi ya Umoja wa Ulaya katika hotuba na taarifa zake.

Vondra anasema watakuwa na furaha iwapo wataweza kukamilisha mambo mawili mahsusi nayo ni masuala ya usalama wa nishati na washirika wa mashariki wa Umoja wa Ulaya.

Serikali ya Czech hivi sasa inaangalia kwa makini juhudi za Urusi na Ukraine kufikia makubaliano juu ya dola bilioni mbili za madeni ya gesi yasiolipwa.

Kampuni ya gesi ya Urusi ya Gazprom imeonya kwamba iitakata usambazaji wake wa gesi kwa Ukraine iwapo madeni hayo hayatolipwa kwa kusema kwamba mkataba mpya unatakiwa uwe umesainiwa ifikapo tarehe Mosi mwezi wa Januari na hakuna mkataba utakaosainiwa bila ya kulipwa kwa fedha hizo.

Kukatwa kwa usambazaji wa gesi kunaweza pia kuathiri watumiaji wa mataifa ya Ulaya ya magharibi ambao hupokea gesi ya Urusi kwa kupitia Ukraine ambao waliathirika kutokana na mzozo huo huo hapo mwaka 2006.

Vondra anasema wakati wa kuwepo kwa hali ya mgogoro nchi ndogo ya Ulaya kama Jamhuri ya Czech ambayo iliwahi kuwa mwanachama wa jumuiya iliokuwa ikiongozwa na Urusi wakati wa enzi iliopita ya ukomunisti inaiwia vigumu kulifanya taifa kubwa la Urusi kusikiliza.

Msimamo wa Czech kwa mazungumzo na Urusi pia umedhoofika kutokana na mvutano wa hivi karibuni juu ya mipango ya Marekani kuweka sehemu ya makombora ya kujihami katika ardhi ya Czech kulikochukuliwa kuwa tishio na Urusi.

Lakini Jamhuri ya Czech bado inapanga kuandaa mkutano wa viongozi wa nchi kati ya Urusi na Umoja wa Ulaya katika miezi sita ya kwanza ya mwaka 2009.

Usalama wa nishati pia litakuwa suala la kujadiliwa katika mkutano wa mawaziri wa mambo ya nje wa Umoja wa Ulaya unaotazamiwa kufanyika mjini Prague hapo tarehe 8 mwezi wa Januari ambao utakuwa mkutano wa kwanza kufanyikla chini ya hatamu za urais wa Umoja wa Ulaya zinazoshikiliwa na Czech.

Katikati ya mwezi wa Desemba Czech ilitangaza kwamba pia ingelipenda kuwa mwenyeji wa mkutano wa viongozi wa Umoja wa Ulaya na Israel sambamba na mkutano wa viongozi wa Umoja wa Ulaya na Wapalestina bila ya kutaja tarehe ya mkutano huo.

Katika kipindi chao cha uongozi wa Umoja wa Ulaya Czech pia inataraji kuwa mwenyeji wa mkutano wa kwanza wa viongozi wa Umoja wa Ulaya na rais mteule wa Marekani Barack Obama,kuanza mchakato wa kuzijumuisha nchi za zamani za muungano wa Kisovieti za Ukraine,Belarus, Armenia.Azerbeijan,Georgia na Moldovia pamoja na kuendelea na mchakato wa kujiunga na Umoja wa Ulaya.