1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wanachama wengi wa SPD wataunga mkono serikali ya mseto

Sekione Kitojo
3 Machi 2018

Mmoja wa viongozi wa ngazi ya juu wa chama cha Social Democratic nchini Ujerumani ametabiri  kwamba asilimia  55 ama zaidi  ya  wanachama wa chama cha SPD wataunga mkono marejeo ya serikali ya mseto na wahafidhina.

https://p.dw.com/p/2tchr
SPD
Picha: picture alliance/dpa/P. Steffen

Wahafidhina wanaoongozwa  na  kansela  Angela Merkel,wataunda serikali pamoja  na  chama  cha  SPD  lakini  kiongozi  huyo  mwandamizi wa  chama  hicho  ameonya  kwamba kura  ya  "hapana" italeta maafa kwa  chama  hicho, Ujerumani  na Ulaya  kwa  jumla.

Thomas Oppermann, makamu  wa  spika  wa  bunge  la  Ujerumani Bundestag, aliliambia  gazeti  la  Die Welt kwamba  anatarajia "uidhinishaji ulio wazi" kwa  kiwango  cha  asilimia  55  katika  kura ya  chama  cha  SPD  iliyopigwa kwa kutumia barua  kupitia  posta zoezi lililomalizika  rasmi  jana  Ijumaa, ambapo  matokeo yatapatikana  kesho Jumapili.

SPD Mitgliederentscheid Große Koalition - Symbolbild
Kura ambayo wanachama wa SPD wamerejesha kwa postaPicha: picture-alliance/dpa/U. Baumgarten

Wanachama  464,000 wa  SPD  wanalazimika  kupiga  kura  juu  ya iwapo waidhinishe uamuzi  wa  viongozi  wa  chama  chao kuendelea  na  kile  kinachofahamika  kama "muungano  mkuu" na wahafidhina  wanaoongozwa  na  kansela Angela  Merkel ambao umeitawala  nchi  hiyo  tangu  mwaka  2013 licha  ya kushindwa  kwa kiasi  kikubwa  kwa  chama  cha  SPD katika  uchaguzi  mkuu  wa taifa  mwezi  Septemba.

Kukataa  ushirikiano mwingine na  vyama  vya  kihafidhina "kutakuwa ni  maafa  makubwa  kwa  Ujerumani, SPD  na  juu  ya  yote , kwa Ulaya," Oppermann  alisema.

Deutschland SPD - Mitgliedervotum
Mwanachama wa SPD akipiga kura yake nyumbaniPicha: picture-alliance/dpa/S. Gollnow

Tawi la  vijana

Tawi la  vijana  la  chama  cha  SPD limekuwa  likipigia  debe wanachama  wake  wapige  kura  ya  hapana  dhidi  ya  kurudiwa kwa  muungano  mkuu, likidai  kwamba  watakuwa  bora  zaidi kujijenga  upya  upande  wa  upinzani  baada  ya  chama  hicho kupata  kipigo  na  kupata  matokeo  mabaya  kabisa  tangu  mwaka 1993  katika uchaguzi  wa  mwezi  Septemba.

Oppermann amewavulia  kofia viongozi  wa  tawi  la  vijana  kwa kuzusha  mjadala  mkubwa  ndani  ya  chama, na  kusema  anatarajia kiongozi  wao, Kevin Kuehnert, ataendelea  kuweka ushawishi  wake katika  chama.

Berlin Angela Merkel, Horst Seehofer und Martin Schulz
Kansela Angela Merkel(katikati) akiwa pamoja na viongozi waliongoza mazungumzo ya kuunda serikali ya mseto. Martin Schulz(kulia)SPD na Horst Seehofer(kushoto)CSUPicha: picture-alliance/dpa/B. von Jutrczenka

Amesema  chama  cha  SPD kinahitaji  "kujiamini  zaidi", kuwa wajanja  kidogo  na  kuwa  tayari  kwa  mizozo" katika  serikali  ya muungano  ijayo.

"Kitisho  kikubwa  zaidi  kitakuwa  kwamba tunarejelea  kile tulichokifanya mara  ya  mwisho," amesema, akionya kwamba mtazamo  wa kinyonge  wa  SPD unaweza  kusababisha  matokeo mabaya  zaidi katika  uchaguzi  baada  ya  miaka  minne.

Chama  cha  SPD awali  kilipanga  kubakia  katika  upinzani, lakini kilikubali kufanya  majadiliano  na  wahafidhina  wanaoongozwa  na Merkel  baada  ya  mazungumzo na  chama  kinachopendelea wafanyabiashara  cha  FDP  na  kile  cha  walinzi  wa  mazingira The Greens katika  muungano  wa  vyama  vitatu kuvunjika  mwezi Novemba.

Deutschland Thomas Oppermann
Makamu spika wa bunge la Ujerumani Thomas Oppermann (SPD)Picha: picture alliance/dpa/K. Nietfeld

Kiongozi  wa  chama  cha  FDP Christian Lindner aliyaambia magazeti  ya  Funke Mediengruppe, kwamba  uchaguzi  mpya utakuwa  suluhisho  bora  zaidi  iwapo  wanachama  wa  SPD watapiga  kura  ya  "hapana". Ameondoa uwezekano  wa  kurejea tena muungano  wa  vyama  vitatu, kutokana  na misimamo  ya vyama  hivyo  vinavyohusika.

Mwandishi: Sekione Kitojo / rtre

Mhariri : Jacob Safari