1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

SPD yapata ushindi wa jimbo la Hamburg

Sekione Kitojo
24 Februari 2020

Chama cha siasa za wastani za mrengo wa kushoto cha SPD, kimeibuka mshindi katika uchaguzi wa jimbo la Hamburg,Ujerumani kikipata asilimia 39 ya kura, kwa mujibu wa matokeo yaliyotolewa na tume ya uchaguzi jana Jumapili.

https://p.dw.com/p/3YHHf
Deutschland Bürgerschaftswahl in Hamburg Peter Tschentscher
Picha: Reuters/C. Mang

Wakati huo huo  inaelekea  wapiga  kura  wamekiadhibu chama  cha kihafidhina cha  kansela Angela  Merkel na  kupata  matokeo mabaya  kabisa  jimboni  Hamburg jana.

Deutschland Bürgerschaftswahl in Hamburg Die Grünen
Chama cha kijani , kimeongeza kupata kura zake mara dufu katika uchaguzi wa HamburgPicha: Getty Images/S. Gallup

Chama  cha  walinzi  wa  mazingira  cha Kijani, chama  ambacho kimekuwa  katika  serikali  ya  muungano  pamoja  na  SPD kwa miaka  mitano  iliyopita  katika  jimbo  hilo, kimechukua  nafasi  ya pili  kikipata  asilimia 24.2, na  kuongeza mara dufu  kura  ilizopata katika  uchaguzi  uliopita  mwaka  2015. Matokeo  hayo  yana maana serikali  ya  muungano  kati  ya  vyama  hivyo inaendelea.

Chama  cha  kansela  Angela  Merkel  cha  Christian Democratic Union, CDU kimepata  matokeo  mabaya  kabisa  ya  bunge  la majimbo  kwa  zaidi  ya  miaka  70, kikipata  asilimia  11.2 tu  ya kura.

Chama  cha  siasa  kali  za  mrengo wa  kushoto  cha  Die Linke , kimefanikiwa  tu  kuongeza  idadi  ya  asilimia  ya  kura   zake  kutoka asilimia  8.5  hadi  asilimia  9.1.

Bürgerschaftswahl - CDU
Chama cha CDU kimepoteza kura nyingi katika uchaguzi wa HamburgPicha: picture-alliance/dpa/D. Reinhardt

Chama  cha  siasa  kali  za  mrengo  wa  kulia  cha  Alternative for Germany , chama  mbadala  kwa  Ujerumani ,AfD kimepata  asilimia 5 na  kile  kinachopendelea  wafanyabiashara  cha  Free  Democrats FDP  kimepata  asilimia  5.3, na  kujihakikishia  kupata  uwakilishi bungeni.

Chama cha  AfD

Katika  uchaguzi  wa  mwaka  2015 chama  cha  AfD kilipata  asilimia 6.1 ya  kura  na  kilishuhudiwa  kikiingia  katika  bunge  kwa  mara ya  kwanza  katika  upande  wa  magharibi  nchini  Ujerumani, lakini kabla  ya  hapo  kilikuwa  kina uwakilishi  katika  majimbo  ambayo yalikuwa  ya  iliyokuwa Ujerumani mashariki  ya  zamani. Chama hicho  sasa  kinauwakilishi  katika  majimbo  yote 16  ya  Ujerumani.

Chama  cha  kihafidhina  cha  Christian Democratic Union , CDU kimepata kipigo  baada  ya  kiongozi  wa  chama  hicho  na mteule wa  kansela  Merkel  Annegret Kramp-Karrenbauer kusema atajiuzulu, na  kufungua  mbio  za  kuwania  kurithi  kiti  cha  kansela na  kukitumbukiza  chama  hicho  katika  mtafaruku.

Bürgerschaftswahl - AfD
Mwanasiasa wa chama cha AfD Kryzysztof Walczak (kushoto) na Alexander Scholz wakifurahia kuingia katika bunge la HamburgPicha: picture-alliance/dpa/F. Molter

Hii  ni  kutokana  na hali  iliyojitokeza  katika  uchaguzi  wa  jimbo  la Thuringia, ambapo  chama hicho  kilijaribu kukaribiana  na chama cha siasa kali za  mrengo  wa  kulia  cha  AfD  katika  uchaguzi  wa  jimbo hilo  la  mashariki  na  hali  hiyo imekitumbukiza  chama  cha  hicho katika  mpambano  wa  kuwania  madaraka. Wanachama waandamizi wa  chama  hicho  wanakutana  leo Jumatatu  kuamua kuhusu  mpango  wa uongozi  mpya wa  chama  hicho , baada  ya kushindwa  vibaya  katika  uchaguzi  wa  Hamburg hali  inayozidi kuleta  dharura  ya  kusaka haraka  uongozi wa  juu  wa  chama hicho.

Mwandishi: Sekione Kitojo / rtre / dpae

Mhariri: Yusuf Saumu