Rais wa zamani wa Afghanistan ameuawa
21 Septemba 2011Mshambuliaji huyo alieficha miripuko chini ya kilemba chake, alikaribishwa nyumbani kwa Rabbani baada ya kujitambulisha kama mjumbe alietumwa na waasi. Rabbani alikuwa Mwenyekiti wa Baraza Kuu la Amani linalotafuta suluhisho la amani pamoja na Wataliban.
Viongozi wa kimataifa wamelaani mauaji ya rais wa zamani wa Afghanistan. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amesema analaani vikali shambulio lililofanywa dhidi ya watu wanaotafuta amani Afghanistan.
Rais wa Ufaransa Nicolas Sarkozy, ameyaeleza mauaji hayo kama ni kitendo cha "uoga usiovumilika" wakati Waziri wa Mambo ya nchi za Nje wa Uingereza, William Hague akisema, mauaji hayo kamwe hayatodhoofisha azma ya serikali ya Afghanistan kupigania amani na upatanisho.
Rabbani alikuwa rais wa Afghanistan kuanzia mwaka 1992 mpaka 1996, alipopinduliwa na Wataliban. Tangu mwaka mmoja uliopita, Rabbani alikuwa akiliongoza Baraza Kuu la Amani linalotafuta suluhisho la kisiasa pamoja na waasi. Yeye ni mwanasiasa wa ngazi ya juu kabisa kuuawa, tangu nchi hiyo ilipovamiwa na majeshi ya kimataifa chini ya uongozi wa Marekani mwaka 2001.