KHARTOUM: Sudan yamfukuza kiongozi wa shirika la misaada la CARE
27 Agosti 2007Matangazo
Sudan imemfukuza kiongozi wa shirika la misaada la CARE lenye makao yake nchini Marekani. Mkurugenzi wa shirika hilo nchini Sudan. Paul Barker, amesema tume ya serikali ya Sudan inayosimamia misaada ya kiutu, imempa muda wa saa 72 aondoke nchini humo.
Hakuna sababu yoyote iliyotolewa na serikali ya Sudan kuhusu uamuzi huo. Barker ni raia wa tatu wa kigeni wa ngazi ya juu kufukuzwa kutoka Sudan katika kipindi cha chini ya wiki moja.
Alhamisi iliyopita Sudan iliwaamuru wanadiplomasia kutoka Canada na Umoja wa Ulaya waondoke, lakini baadaye ikamruhusu balozi wa umoja huo abaki mpaka awamu yake ya ubalozi itakapomalizika mwezi ujao.
Maafisa wa tume ya Sudan inayoshughulikia utoaji wa misaada ya kiutu hawajasema lolote.