1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

JERUSALEM: Mawaziri wa kigeni wa Misri na Jordan wawasili Jerusalem

25 Julai 2007
https://p.dw.com/p/CBfR

Mawaziri wa kigeni wa Misri na Jordan wamewasili nchini Israel mapema leo kwa mazungumzo juu ya mpango wa amani ya Mashariki ya Kati wa jumuiya ya nchi za kiarabu.

Msemaji wa wizara ya kigeni ya Israel amesema mazungumzo hayo yatajadili mpango wa amani uliopendekezwa kwanza kwenye mkutano wa jumuiya ya nchi za kiarabu mjini Beirut nchini Lebanon mnamo mwaka wa 2002.

Mpango huo unapendekeza kurudisha mahusiano ya kawaida kati ya Israel na mataifa yote ya kiarabu ikiwa Israel itaondoka kutoka maeneo inayoyakalia, kukubali kuundwa kwa taifa huru la Palestina na kutafuta suluhisho kwa tatizo la wakimbizi.

Ziara ya mawaziri wa kigeni wa Misri na Jordan inafanyika kufuatia ziara ya kwanza ya waziri mkuu wa zamani wa Uingereza, bwana Tony Blair, katika Mashariki ya Kati.

Blair alikutana na viongozi wa Palestina na waziri mkuu wa Israel Ehud Olmert. Olmert amesema atashirikiana na Blair.

´Nitafana kila juhudi kushirikiana naye na kutazama mbele vipi mambo yanavyoweza kufanywa kwa pamoja ili kuwapa Wapalestina fursa ya kweli kuwa na taifa lao.´

Tony Blair amesema ziara yake ilikuwa fursa kusikiliza na kujifunza na akazungumzia kuhusu uwezekano wa kufikia mafanikio katika eneo hilo.