1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Je, Umoja wa Ulaya utamshinikiza Modi kuhusu Ukraine?

2 Mei 2022

Waziri Mkuu wa India Narendra Modi anaizuru Ulaya. Katika mkutano wake wa kwanza kabisa na Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz Jumatatu, wataongoza kikao cha Mashauriano baina ya Ujerumani na India, IGC, mjini Berlin.

https://p.dw.com/p/4AhGr
Indien | Tag der Republik | Premierminister Narendra Modi
Picha: Adnan Abidi/REUTERS

Katika ziara yake hii, Modi anatafuta kuimarisha mahusiano na nchi za Ulaya na wakati huo huo kuonyesha msimamo wa India wa kutoupendelea upande wowote katika vita vya Urusi na Ukraine.

Tangu kuanza kwa vita vya Urusi na Ukraine, India imejitenga na kuvituhumu vitendo vya Urusi huku ikizidi kuyanunua mafuta ya Urusi kwa wingi, kinyume na bara la Ulaya ambalo linajaribu kujiondoa kutoka kwenye utegemezi wa nishati ya Urusi huku likiongoza kampeni ya mataifa mbalimbali ya kupinga vita hivyo.

Je, Modi atashinikizwa kuhusu msimamo wake wa vita vya Ukraine?

Katika ziara hii Modi anatarajiwa kuwaeleza viongozi wa Ulaya, msimamo wa India kwa Ukraine. Lakini swali kuu ni je, iwapo msimamo huo utakuwa kinyume na wa Ulaya, hakutokuwa na shinikizo lolote?

Katika kipindi cha mwezi mmoja uliopita, kumekuwa na ziara nyingi za maafisa wa nchi za Magharibi kuelekea India na katika ziara hizo wamejitahidi hawajamshinikiza Modi kulaani vita vilivyoanzishwa na Urusi. Wiki iliyopita, Rais wa Halmashauri Kuu ya Umoja wa Ulaya Ursula von der Leyen alifanya mkutano na Waziri Mkuu Modi ambapo walikubaliana kuhusiana na ushirikiano mpya wa kibiashara na teknolojia na wakaahidiana kuuzidisha uhusiano kati ya India na Ulaya.

India EU
Rais wa Halmashauri Kuu ya Umoja wa Ulaya Ursula von der Leyen akiwa na Waziri Mkuu ModiPicha: dpa/picture alliance

Wiki hiyo hiyo Modi pia alikutana na Waziri Mkuu wa Uingereza Boris Johnson na waziri wa mambo ya nje wa India Harsh Vardhan Shringla akasema kiongozi huyo hakushinikizwa kivyovyote vile kuhusiana na msimamo wa nchi yake kwa uvamizi wa Urusi.

Mnamo mwezi Machi, mshauri wa masuala ya kigeni na usalama wa Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz, Jens Plötner, alikutana na mshauri wa kitaifa wa usalama nchini India Ajit Doval na baada ya mkutano wao akasema Ujerumani haitozungumza na India kuhusiana na vita vya Ukraine.

India ni mshirika mkuu wa Ujerumani na Umoja wa Ulaya katika biashara

Ifahamike kwamba India ni mshirika wa kimkakati wa Umoja wa Ulaya na ndiyo mshirika wa tatu mkuu wa kibiashara huku ikiwa mwaka wa 2020 pekee, biashara kati ya Ulaya na India ilipindukia dola bilioni 66. Ikumbukwe pia kwamba India nchi ya pili inayonunua bidhaa za Umoja wa Ulaya kwa wingi duniani baada ya Marekani.

Indien Treffen Wladimir Putin und Narendra Modi
Rais wa Urusi Vladimir Putin na Waziri Mkuu Narendra Modi wa IndiaPicha: Money Sharma/AFP/Getty Images

Baada ya kutoka Berlin, Waziri Mkuu Modi atasafiri na kuelekea Copenhagen ambapo amealikwa na Waziri Mkuu wa Denmark Mette Frederiksen kushiriki katika mkutano wa kilele wa India na nchi za nordic ambapo atakutana pia na viongozi wa Iceland, Norway, Sweden na Finland.

Kituo chake cha mwisho kitakuwa mjini Paris ambapo atakutana na Rais Emmanuel Macron wa Ufaransa.

 LINK: https://www.dw.com/a-61633736