1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Nchi tatu za Ulaya zaitambua Palestina kama dola huru

22 Mei 2024

Ireland, Uhispania na Norway zimetangaza mipango ya kuitambua Palestina kama dola huru. Israel imepinga vikali hatua ya nchi hizo tatu za Ulaya.

https://p.dw.com/p/4g8eJ
Mji wa  Gaza | Wapalestina wakimbia vita
Wapalestina waondoka kwenye makazi yao kwenda kwenye sehemu salama wakikimbia vita katika eneo la Zeitoun kwenye Ukanda wa GazaPicha: Dawoud Abo Alkas/Anadolu/picture alliance

Hatua ya nchi hizo inavunja msimamo ulioshikiliwa kwa muda mrefu na nchi za Magharibi kwamba taifa huru la Palestina linaweza tu kupatikana kwa kuyafanikisha mazungumzo ya amani kati ya mamlaka ya Palestina na Israel.

Waziri Mkuu wa Ireland Simon Harris aliwaambia waandishi wa habari kwamba siku ya Jumatano tarehe 21/05/2024 ni siku muhimu na ya kihistoria kwa nchi yake na kwa watu wa Palestina.

Pedro Sanchez alipozuru Ireland
Kushoto: Waziri Mkuu wa Ireland Simon Harris. Kulia: Waziri Mkuu wa Uhispania Pedro SanchezPicha: Brian Lawless/PA Wire/empics/picture alliance

Ireland, Norway na Uhispania zilisema zitaitambuwa  rasmi Palestina kama dola huru mnamo Mei 28.

Waziri Mkuu wa Norway Jonas Gahr Store amesema amani haiwezi kuwepo katika eneo la Mashariki ya kati iwapo Palestina haitatambuliwa.

Soma Zaidi: Uhispania kuitambua Palestina kama taifa huru 

Chama cha Ukombozi wa Palestina, PLO kinachotambulika kimataifa kama ndio mwakilishi pekee halali wa watu wa Palestina, kimepongeza uamuzi wa kihistoria wa leo Jumatano uliotangazwa nchi tatu za Ulaya wa kulitambua taifa la Palestina. Kundi la Hamas linalotawala katika eneo la Ukanda wa Gaza pia limeipongeza hatua hiyo.

Kutokana na hatua hiyo iliyochukuliwa na Norway, Ireland na Uhispania ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Israel, Katz Israel, amewaamuru mara moja mabalozi wake kutoka Norway na Ireland kurejea nyumbani. Amesema hatua kama hiyo pia itachukuliwa kwa balozi wa Israel wa nchini Uhispania.

Israel Katz
Waziri wa Mambo ya Nje wa Israel, Katz Israel,Picha: Lev Radin/Pacific Press/picture alliance

Israel imepinga vikali hatua hiyo, ikisema kuwa ni sawa na ugaidi baada ya kundi la wanamgambo wa Hamas kufanya mashambulizi katika ardhi ya Israel mnamo Oktoba 7 mwaka uliopita.

Waziri huyo wa Mambo ya Nje wa Israel amezilaumu Norway, Ireland na Uhispania kwa kwa kuchukua hatua ambayo ameiita kuwa inawanyima haki watu walioathiriwa na mashambulizi ya Hamas ya mwaka jana.

Soma Zaidi:Israel yaapa kuendeleza operesheni ya Rafah dhidi ya Hamas

Serikali za Magharibi na Marekani zasemaje

Hata hivyo serikali nyingi za Magharibi ikiwa ni pamoja na Marekanizinasema ziko tayari siku moja kuitambua Palestina kama taifa huru ingawa zimesema hazitafanya hivyo kabla ya makubaliano kufikiwa kuhusu masuala yenye utata kama vile mipaka kati ya Israel na Palestina pamoja na swala linalohusu hadhi ya mji wa Jerusalem.

Vyanzo: AFP/RTRE/AP/DW