1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Janga

Covid-19: Merkel aonya dhidi ya kuondoa vizuwizi kwa pupa

Iddi Ssessanga
20 Aprili 2020

Wakati maduka madogomadogo yameruhusiwa kufungua nchini Ujerumani, kansela Angela Merkel amesema inaweza kuwa kosa kuendelea kwa haraka, na kuwataka raia waendelee kuheshimu hatua za kujitenga.

https://p.dw.com/p/3bBT6
Deutschland Berlin Coronavirus - Pressekonferenz Angela Merkel
Picha: picture-alliance/AP/M. Schreiber

Kansela wa Ujerumani Angela Merkel amewatolea wito raia na wakaazi kuendelea kuheshimu hatua za kukaa mbalimbali, akisema itakuwa aibu kubwa iwapo watajikwaa na kurudi katika mripuko huku wakiona.

Mapema Jumatatu, baadhi ya majimbo ya Ujerumani yalilegeza vikwazo vilivyowekwa kudhibiti mripuko wa virusi vya corona, ikiwemo kufungua kwa sehemu maduka. Ameyatahadharisha majimbo dhidi ya kulegeza zaidi vikwazo hivyo.

"Tumesima mwanzoni mwa janga na bado tuna safari ndefu ya kuondoka kwenye hali hiyo," alisem Merkel.

Kansela huyo pia alibainisha kwa bajeti ijayo ya Umoja wa Ulaya huenda ikafanyiwa marekebisho kuhakikisha ufufukaji mkubwa wa kiuchumi kufuatia janga la corona.

"Tutahitaji mjibu ya haraka kushughulikia janga hili na Ujerumani itataraji katika majibu ya mshikamano unaokwenda mbali ya euro bilioni 500 ($543 bilioni) tulizo nazo kwa sasa," alisema.

BG Deutschland Corona Lockerung
Bango linalosomeka "Tumerudi" Tumefurahi kukuona tena" likining'inia kwenye duka mjini Ludwigsburg, Aprili 20, 2020, wakati biashara zikianza kufungua polepole nchini Ujerumani.Picha: Getty Images/AFPT. Keinzle

Ujerumani inashika nafasi ya tano kwa kuwa visa vingi vya maambukizi ya covid-19 duniani nyuma ya Marekani, Uhispania, Italia na Ufaransa, ikiwa na visa zaidi ya 145,000 lakini vifo nchini humo vimealia kuwa chini kwa 4,642, kwa sehemu kutokana na upimaji wa mapema na mpana.

China yavaliwa njuga na mataifa kuhusu mripuko

Merkel aliwaambia waandishi habari kwamba China inahitaji kuwa muwazi zaidi kuhusu namna ilivyoshughulikia mripuko, na kusema itakuwa "bora kwa wote."

Wanasayansi nchini China wanasema kuna uwezekano mkubwa maambukizi ya kwanza ya virusi hivyo yalitokea kwa wanadamu kwenye soko la wanayama hai wa porini.

Lakini dhana zisizothibitishwa kwamba kirusi hicho kilitoka kwenye maabara yenye ulinzi mkali ya virusi mjini Wuhan, zimeibuliwa na baadhi ya maafisa wa Marekani, akiwemo waziri wa mambo ya nje Mike Pompeo, aliesema uchunguzi unafanyika kuhusu namna virusi hivyo "vilivyoingia duniani."

Taasisi ya virusi vya Wuhan imekanusha vikali madai kwamba inaweza kuwa chanzo cha mripuko huo, ikisema ni jambo "lisilowezekana."

China Wuhan Coronavirus Institute of Virology
Maabara ya P4 katika chuo cha virolojia cha Wuhan katika mkoa wakati wa Hubei, ambamo inadaiwa huenda kirusi cha corona kilitengenezwa.Picha: Getty Images/AFP/H. Retamal

Maafisa wa serikali ya China wametuhumiwa kwa kupuuza mrpuko awali, na wiki iliyopita, maafisa mjini Wuhan walikiri kufanya makosa katika kuhesabu idadi yao ya vifo na kurekebisha tarakimu zake kwa asilimia 50.

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron wiki iliyopita aliliambia gazeti la Financial Times itakuwa "ujinga" kudhani kwamba China ilishughulikia vyema janga hilo, na kuongeza: "Ni wazi kuna mambo yaliotokea ambayo hatuyajui."

Nchini Uingereza, waziri wa mambo ya nje Dominic Raab alisema China itakabiliwa na "madhara magumu" kuhusu mripuko wa virusi vya corona, ambayo ni "namna vilivyokuja na namna ambavyo visingiweza kudhibitiwa mapema."

Australia wakati huo huo imetoa wito wa kufanyika uchunguzi huru katika hatua za dunia dhidi ya mripuko huo, ikiwemo namna shirika ka afya duniani lilivyoshughulikia mzozo huo.

Waziri wake wa mambo ya nje amesema taifa hilo "litasisitiza" juu ya ukaguzi utakochunguza, kwa sehemu, hatua zilizochukuliwa na China baada ya kuzuka kwa mripukohuo.

Chanzo: afpe,DW