1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

SPD wasaka mshirika serikalini

16 Februari 2015

Shangwe zimehanikiza tangu Hamburg hadi makao makuu ya chama cha SPD mjini Berlin.Baada ya ushindi katika uchaguzi wa jiji la Hamburg diwani mkuu Olaf Scholz anapewa nafasi ya kuvaa taji la uongozi wa taifa

https://p.dw.com/p/1EcGz
Fashi fashi katika bandari ya HamburgPicha: picture-alliance/dpa/Angelika Warmuth

Baada ya uchaguzi huo wa jana,vyama vya kisiasa katika mji huo mashuhuri wa kaskazini na mjini Berlin vimeanza kuzungumzia matokeo yake.Chama cha SPD kimejipatia ushindi bayana kwa mara ya kwanza toka jumla ya chaguzi mbili za majimbo mwaka huu.Baada ya miaka minne kudhibiti hatamu za uongozi ,hivi sasa Olaf Scholz na chama chake cha SPD wanahitaji mshirika serikalini.Walinzi wa mazingira,ambao Scholz anasema angependelea kushirikiana nao madarakani wameshasema majadiliano ya kuunda serikali ya muungano yatakuwa magumu.

Chama cha Christian Democratic cha kansela Angela Merkel kimepata pigo kubwa.Waliberali wa FDP wamefanikiwa kukiuka kiunzi cha asili mia tano sawa na chama kipya Chaguo Mbadala kwa Ujerumani AfD kilichojikingia asili mia sita nukta moja na kuwakilishwa kwa mara ya kwanza katika bunge la Hamburg.

Mwenyekiti wa kundi la wabunge wa chama cha SPD,Thomas Oppermann anayaangalia matokeo ya uchaguzi wa jana huko Hamburg kama ishara njema kwa chama chao.

Ahadi za uchaguzi zitatekelezwa

Mweyewe Olaf Scholz anasema:"Huu ni ushahidi wa imani ya wakaazi wa jiji hili na ndio maana nnasema "Ahsanteni sana kwa kuniamini,na kwa kuniunga mkono.Hatutakuvunjeni moyo.Jukumu mlilotutwika tutalitekeleza.Nyote katika jiji hili la Hamburg mnaweza kutuamini."

Deutschland Bürgerschaftswahl in Hamburg
Mwenyekiti wa chama Mbadala kwa Ujerumani-AfD Bernd Lücke na mgombea wa chama hicho jijini Hamburg Jörn Kruse(kulia)Picha: picture-alliance/dpa/M. Christians

Olaz Scholz anakwenda Berlin hii leo kwa mazungumzo pamoja na mwenyekiti wa cha cha SPD Sigmar Gabriel.Kutokana na ushindi wake huo wa pili,diwani mkuu wa Hambourg amepata nguvu katika daraja ya shirikisho.Hakuna katika uongozi wa SPD anaeweza kushindana nae kwa kujikingia wingi wa kura.Na kutokana na makadirio haba ya maoni ya wananchi kwa chama cha SPD sauti zimeshaanza kupazwa kama Sigmar Gabriel akiwakiliashe kweli chama chao katika uchaguzi mkuu mwaka 2017.

FDP washusha pumzi

Kwa mujibu wa matokeo ya awali,SPD wamejikingia asili mia 45,7-wamepungukiwa na kura kidogo ikilinganishwa na uchaguzi wa mwaka 2011.CDU kimepoteza asili mia 6 na kusaliwa na asili mia 15.9-matokeo mabaya kabisa kuwahi kujipatia chama hicho jijini Hamburg.Walinzi wa mazingira wamejiimarisha na kujikingia asili mia 12.2.Chama cha FDP kimefanikiwa kwa mara ya kwanza tangu kilipopigwa kumbo katika daraja ya taifa,kusalia katika bunge la jimbo kwa kujikingia asili mia 7.4.Huku chama cha siasa kali za mrengo wa kushoto die Linke kikijijenga kwa asili mia 8.4.

Bürgerschaftswahl in Hamburg Katja Suding
KIoozi wa chama cha FDP Hamburg Katja Suding (Kati)Picha: picture-alliance/dpa/B. Marks

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/dpa/AFP

Mhariri : Mohammed Abdul-Rahman