1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Vladimir Putin amemteuwa Viktor Subkov awe waziri mkuu mpya wa Russia

13 Septemba 2007

Jana Rais wa Russia, Vladimir Putin, alimwachisha kazi waziri mkuu wa nchi hiyo, Michael Fradkow, na kumpendekeza bingwa wa masuala ya fedha, Viktor Subkov, kukamata nafasi hiyo.

https://p.dw.com/p/CB1H
Viktor Subkov, akiyeteuliwa na Rais Putin kuwa waziri mkuu mpya wa Russia
Viktor Subkov, akiyeteuliwa na Rais Putin kuwa waziri mkuu mpya wa RussiaPicha: AP

Kutoka ile kofia ambayo rais wa Russia, Vladimir Putin , alikuwa anaitumia kufanyia mazingaombwe, amechomza sungura, na jina la sungura huyo ni Viktor Subkov. Kama kawaida: mazingaombwe hayo yanapomalizika kufanywa, watu hubakia kuguna na kushangaa wakisemasema Ahh na Ihh. Nani huyu Subkov? Watu wengi hawamjui. Yeye ni bingwa wa masuala ya fedha, tena ni msiri wa Vladimir Putin tangu zamani walipokuwa pamoja katika mji wa St. Petersburg. Sio mtu aliyejitokeza sana hadharani, ni mtu wa safu ya pili. Ni mtu ambaye ni taabu kuelezea wasifa wake.

Labda hayo sio muhimu sana. Lililo muhimu ni kwamba Vladimir Putin ameonesha kwa watu wote nani aliye Bosi. Yeye ni mwanasiasa ambaye huwaacha watu na vitandawili, huwafunika watu macho, huku akiendeleza mkakati wake; hodari wa kusababisha mishangao na kuifanya dunia nzima itambuwe kwamba kuna mtu mmoja tu aliye na usemi wa juu kabisa katika siasa za ndani za Russia. Naye ni Vladimir Vladimirowitsch Putin; Rais ambaye ana historia ya kuwa kada wa shirika la ujasusi la Urussi ya zamani, KGB.

Mwezi Machi mwakani, mhula wake wa urais kwa mara ya pili utamalizika. Lakini hata baada ya hapo, lazima watu wamtie katika hesabu, hatachoka, bado atavuta pumzi. Vladimir Putin tangu sasa anajisafishia njia baada ya yeye kuwacha madaraka mwakani. Mambo katu hayatamwendea vibaya.

Kwa kumteuwa bingwa huyo wa masuala ya fedha, Viktor Subkov, mtu ambaye hana bashasha, rais Putin anataka kuonesha kwamba mtu hiyo anafaa kuongoza mustakbali wa nchi hiyo kubwa ambayo inajionea na mafanikio makubwa ya kiuchumi lakini pia mamatizo makubwa ya kisiasa. Watu anaowafikiria yeye kuongoza ni wale waliokuwa zamani makachero, maafisa wenye ujuzi wa utawala, wasiojishughulisha na siasa, watu wasiovutia, mabingwa wa mambo yeyote, kama ni kilimo, jeshi au masuala ya fedha, lakini sio wale watu walio na uzoefu, wenye bashasha au wanasiasa wenye uhalali uliotokana na kujengwa mawazo ya kisiasa. Watu hao, kwa Putin, wanatafuta zaidi kuliko uchapaji wa kazi. Ndio maana Vladimir Puti akamteuwa mwanasiasa, lakini asiyejishughulisha na siasa.

Kwa nia njema, mtu anaweza kusema hayo yanayopita Mosko ni mambo ya kawaida. Angalau nje ya Russia, sababu ya kufanywa mabadiliko haya ya baraza la mawaziri ni jambo geni. Jee mtu analibadilisha baraza lake la mawaziri kwa sababu tu uchaguzi uko mlangoni? Putin amesema kwamba kabla ya kufanyika chaguzi za bunge na za urais, lazima iundwe serekali ambayo itaweza kuitayarisha nchi kwa ajili ya mabadiliko yanayotarajiwa. Mfumo wa madaraka lazima ujengwe upya. Ajabu. Ikiwa mambo yawe kwa mujibu wa mfumo wa kidemokrasia, ulio huru na haki, basi hapo tena serekali itawataka wananchi waamuwe juu ya kazi iliofanywa na viongozi hao wa serekali- ama kuwabakisha madarakani au kuwaondoa.

Kipindi kabla ya uchaguzi katika Russia ni wakati wa kupikiana majungu ya kisiasa, ulaghai, ujanja na udangayifu. Hayo hayatokuwa na matokeo mazuri.