1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mzozo wa Fedha Marekani-AIG yaokolewa

Jens Korte - (P.Martin)17 Septemba 2008

Kilichotokea wala hakieleweki.Kwani usiku wa kuamkia Jumatano,Shirika la Kimataifa la Bima nchini Marekani AIG,ambalo hadi wiki iliyopita lilikuwa shirika kubwa kabisa la bima duniani,limetaifishwa kwa sehemu kubwa.

https://p.dw.com/p/FJiG
**FILE** Federal Reserve Board Chairman Ben Bernanke pauses while discussing the near-term economic outlook during testimony before the House Budget Committee on Capitol Hill in Washington in this Thursday, Jan. 17, 2008 file photo. (AP Photo/Dennis Cook. File) ***Zu Mir Haschemi, Der Mann hinter dem Leitzins - über Ben Bernanke dem Chef der US Notenbank******Zu Mir Haschemi, Der Mann hinter dem Leitzins - über Ben Bernanky dem Chef der US Notenbank***
Mwenyekiti wa Benki Kuu ya Marekani Ben BernankePicha: AP

Hadi dakika ya mwisho mameneja wa AIG pamoja na Benki Kuu ya Marekani mjini New York walijitahidi kukusanya mtaji.Hata Waziri wa Fedha Henry Paulson na Mkuu wa Benki Kuu ya Marekani Ben Bernanke waliitisha kikao cha dharura mjini Washington.Matokeo yake ni kuwa AIG itapatiwa mkopo wa dola bilioni 85 lakini serikali itadhibiti asilimia 79.9 ya hisa za shirika hilo la bima.Mali ya AIG inatathminiwa kuwa ni kama dola trilioni 1.2 na ina wateja milioni 74 katika nchi 130.Labda ni kwa sababu hiyo hakuna aliejitokeza haraka kulisaidia shirika hilo.Benki mbili kuu pekee za uwekezaji zilizobaki huko Marekani yaani Goldman Sachs na JP Morgan zilijiweka mbali kabisa.Kwa hivyo serikali,shingo upande ikajitolea kulisaidia shirika hilo na hivyo kuzuia maafa makubwa katika masoko ya fedha kote duniani.Kwani pindi AIG ingeachiwa kwenda muflisi basi masoko ya fedha duniani yangetumbukia katika janga kubwa.

Suala linaloulizwa ni vipi mzozo wa mikopo umeweza kuathiri shirika kama AIG?Ukweli ni kuwa shirika hilo la bima lilijitosa katika soko la mikopo iliyodhaminiwa kwa hisa na mikopo ya nyumba na lilipata faida kubwa kuliko kutoa bima za nyumba,maisha au magari.Shirika la AIG lilijikusanyia hati za aina hiyo zilizokuwa na thamani ya kama dola bilioni 400.Matatizo yakachomoza katika sekta ya bima ya mikopo.Kwani katika sekta hiyo mashirika ya bima hukatiana bima dhidi ya hatari ya kutopokea malipo kwa mfano kutoka benki za mikopo ya nyumba.Ikiwa benki haina uwezo wa kulipa madeni yake basi bima zilizodhaminiwa na benki zingine hazina thamani tena.

Na usiku wa Jumatatu kuamkia Jumanne shirika linalopima uwezo wa malipo wa benki,lilipunguza kiwango cha uwezo wa AIG na shirika hilo la bima lilipaswa kutafuta wadhamini lakini hakuna aliejitokeza katika sekta binafsi.Kwa hivyo Washington haikuwa na budi isipokuwa kujitokeza kama mwokozi.

Hivi sasa masoko ya fedha yanapumua kidogo.Lakini kwa hasara gani?Kwani katika kipindi cha siku chache tu,mzozo wa mikopo ya nyumba umeonyesha athari zake kwa yale yaliyofikiwa na benki mbili kuu za uwekezaji Lehman Brothers na Merrill Lynch nchini Marekani na sasa AIG shirika maarufu kabisa katika masoko ya fedha duniani limepoteza uhuru wake.Kwa hivyo masoko ya fedha,benki na wawekezaji wanapaswa kuishukuru serikali ya Marekani kwa hatua iliyochukuliwa kuzuia maafa makubwa katika masoko ya fedha duniani.