Mawingu ya jivu yakorofisha safari za ndege ulimwenguni
19 Aprili 2010Umoja wa Ulaya unafikiria kuruhusu idadi kubwa ya safari za ndege katika anga ya ulaya hii leo baada ya kupooza kwa muda wa siku nne kufuatia mawingu ya jivu kutoka katika mlima wa volkano wa Island.Mamilioni ya abiria wamekwama kote ulimwenguni.
Wakitiwa kishindo na makampuni ya ndege yanayohisi vizuwizi vilivyowekwa dhidi ya safari za ndege katika anga la nchi za ulaya vimefurutu,mawaziri wa usafiri wa Umoja wa Ulaya wanashiriki kwa njia ya video katika mkutano wa dharura hii leo kuzungumzia suala hilo.
Lakini kuna kila dalili kwamba maabria watalazimika kupitisha siku ya tano katika viwanja vya ndege vya nchi kadhaa za Ulaya hii leo ,ambako baadhi ikiwa ni pamoja na Ujerumani,Uholanzi na Ubeligiji zimeshasema viwanja vya ndege havitafunguliwa kabla ya saa tatu za usiku kwa saa za Afrika Mashariki-mfano nchini Ujerumani na Ubeligiji.
Viwanja viwili vya ndege vimefunguliwa tangu leo asubuhi nchini Rumania na vyengine viwili nchini Finland.
Uamuzi wa kufunga viwanja vya ndege na kuzuwia safari za ndege uliosababishwa na mawingu ya jivu kutoka mlima wa Volkano wa EYJAFJÖLL nchini Island umewalazimisha abiria milioni sita na laki nane kukwama katika viwanja vya ndege 313 kote ulimwenguni.
Halmashauri kuu ya Umoja wa Ulaya ilitaka kuruhusu upya safari za ndege kuanzia wiki hii,kufuatia shinikizo la makampuni ya safari za ndege yanayotaka kwa kila hali kujikwamua toka janga hili lililosababisha hasara ya yuro milioni 147,na laki tatu hadi leo.
Waziri wa usafiri wa serikali kuu ya Ujerumani Peter Ramsauer aneondowa uwezekano wa kulipwa fidhia makampuni ya safari za ndege.Akihojiwa na kituo cha matangazo cha Deutschlandfunk bwana Ramsauer amesema atapinga uamuzi wowote wa kuigeukia serikali.Waziri wa usafiri wa serikali kuu ya Ujerumani amesema ya fedha iliyosababishwa na janga la mawingu ya jivu inahitaji kutathminiwa,lakini anasema tunanukuu:"Mbali na sekta zilizoathirika na janga hili,kuna nyengine zinazofaidika sana"Mwisho wa kumnukuu waziri wa usafiri aliyesisitiza "usalama wa abiria ni muhimu kuliko kitu chochote chengine."
Mashirika matatu ya safari za ndege,ikiwa ni pamoja na Lufthansa la Ujerumani yalifanya utafiti kutathmini hali namna ilivyo angani.
Kepteni wa Lufthansa Werner Knorr anasema
"Kitu pekee ambacho hakikua cha kawaida ni ile hali kwamba sisi tulikua peke yetu kutoka na madege makubwa makubwa nchini Ujerumani."
Mkurugenzi wa shirika la kimataifa la usafiri wa ndege IATA ,Giovanni Bisignani amekosoa vikali jinsi Umoja wa Ulaya unavyoshughulikia mzozo wa mawingu ya jivu ya mlima wa volkano wa Island.
Mwandishi: Hamidou, Oummilkheir /rtr/afp/dpa
Mpitiaji: Abdul-Rahman, Mohammed