1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroMarekani

Marekani kuisaidia Ukraine kwa taarifa za kijasusi

2 Oktoba 2025

Gazeti la The Wall Street Journal limeripoti kuwa Marekani inapanga kuipa Ukraine taarifa za kijasusi zitakazotumika kuratibu mashambulizi ya makombora ya masafa marefu dhidi ya miundombinu ya nishati ya Urusi.

https://p.dw.com/p/51Nal
Ukraine 2025 | Mwanajeshi wa Ukraine | Droni
Mwanajeshi wa Ukraine akifanya jaribio la kurusha droniPicha: Yevhen Titov/AP Photo/dpa/picture alliance

Kwa mujibu wa gazeti la The Wall Street Journal, maafisa wa serikali ya Marekani wamenukuliwa wakieleza kuwa hatua hiyo inazingatiwa wakati Washington ikitathmini uwezekano wa kuipatia Kyiv silaha zaidi zenye uwezo wa kushambulia kwa umbali mrefu.

Licha ya kwamba Marekani imekuwa ikishirikiana na Ukraine kwa muda mrefu katika kubadilishana taarifa za kijasusi, ripoti hiyo inaeleza kuwa mpango huo mpya unaweza kuirahisishia Ukraine kushambulia viwanda vya kusafisha mafuta, mabomba ya gesi, vituo vya umeme, na miundombinu mingine muhimu—kwa lengo la kuinyima Urusi mapato ya nishati.

Gazeti hilo limeongeza kuwa maafisa wa Marekani pia wanawahimiza washirika wa jumuiya ya NATO kuunga mkono hatua hiyo kwa kutoa msaada wa aina hiyo kwa Ukraine.

Hata hivyo, Ikulu ya White House haikujibu mara moja ombi la kutoa maoni kuhusu taarifa hizo.