1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni ya wahariri juu ya Syria,Brics

Abdu Said Mtullya27 Machi 2013

Wahariri wanazungumzia juu ya mgogoro wa Syria mkutano wa nchi zinazoinukia kiuchumi na pia wanatoa maoni yao juu ya msako uliofanywa katika asasi za kutetea demokrasia nchini Urusi.

https://p.dw.com/p/184to
Mawaziri wa"Brics"wakutana Afrika Kusini
Mawaziri wa "Brics" wakutana Afrika KusiniPicha: picture-alliance/dpa

Juu ya mgogoro wa Syria mhariri wa gazeti la "Westfalen-Blatt" anaitilia maanani dhima ya Marekani katika mgogoro huo. Anasema Marekani inawania kuwa mstari wa mbele. Mhariri huyo anakumbusha juu ya kauli ya Rais Obama ya hivi karibuni kwamba, ikiwa itabainika kuwa utawala wa Assad umezitumia silaha za kikemia, sera ya Marekani juu ya mgogoro wa Syria itabadilika.

Mhariri wa gazeti la "Westfalen-Blatt" anasema kauli hiyo ni nzito.Hata hivyo mhariri wa gazeti hilo anaeleza kwamba, wakati sera rasmi ya Marekani hairuhusu kuwapelekea silaha wapinzani wa Assad,katika pembe za chaki shehena za silaha za Marekani zimekuwa zinapelekwa kwa ndege za nchi hiyo.

Lakini mhariri wa"Westfalen-Blatt" anaitahadharisha Marekani kwamba ikiwa, inakusudia kuwa na dhima muhimu nchini Syria baada ya Assad kuondolewa lazima ijitokeze mbele zaidi.

Benki ya Maendeleo ya BRICS

Gazeti la"Osnabrücker linatoa maoni juu ya mkutano wa nchi zinazoinukia kiuchumi duniani,"Brics", unaofanyika, Durban nchini Afrika Kusini. Mhariri wa gazeti hilo anaamini kwamba nchi hizo bado zipo mbali na ndoto ya kuwepo mfumo mpya wa dunia.Anasema kwa nchi zinazoinukia kiuchumi kuwa kitovu cha mfumo mpya wa dunia,kama Urusi inavyotamani,bado pana njia ndefu. Ustawi wa uchumi unapungua katika nchi hizo, japo bado ni wa juu kulinganisha na ule wa nchi za magharibi. Wawekaji vitega uchumi bado wanapendelea kuekeza fedha katika nchi kama Ufilipino, Nigeria au kwa mshirika wa miaka mingi- Japan. Pamoja na hayo, ubashiri kwamba,Marekani itapitwa katika nguvu za kiuchumi, bado haujathibiti kuwa wa kweli hadi sasa.

Na kwa hivyo, mhariri wa "Osnabrücker "anasema, habari kwamba, nchi zinazoinukia kiuchumi zinaunda benki yao ya maendeleo, hazipaswi kuwa za kushtusha sana. Nchi hizo hazitafanikiwa haraka katika lengo hilo.

Ujerumani yalalamika:

Serikali ya Ujerumani imelalamika kwa Urusi juu ya msako uliofanywa katika ofisi za Wakfu wa Ujerumani,Konrad Adenauer,katika mji wa St Petersberg nchini Urusi.

Juu ya kupekuliwa kwa ofisi za Wakfu huo,gazeti la "Handelsblatt" linasema watawala wa Urusi wana hofu kufuatia maandamano makubwa yaliyofanywa na wananchi mwaka uliopita dhidi yao. Watawala hao wanahofia kuwapo kwa jamii ya kisasa ambamo wananchi wana usemi. Na mhariri wa "Lübecker Nachrichten" anaeleza kuwa hatua ya idara ya usalama ya Urusi kuzipekua ofisi za Wakfu wa Ujerumani nchini humo,yumkini inatokana na msimamo wa Ujerumani wa kutetea hoja ya kuzitoza kodi fedha za Mafia wa Kirusi zilizowekwa katika benki za nchini Cyprus.

Mwandishi:Mtullya abdu./Deustche Zeitungen/

Mhariri: Yusuf Saumu