1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

COLOMBO: Ngome ya waasi wa Tamil Tigers yashambuliwa

18 Oktoba 2006
https://p.dw.com/p/CD1g

Ndege za jeshi la Sri Lanka zimeishambulia ngome ya waasi wa Tamil Tigers mashariki mwa nchi hiyo mapema leo. Mwanamke mmoja ameuwawa na watu kadhaa wamejeruhiwa katika shambulio hilo lililofanywa katika kijiji cha Thalaichenai katika wilaya ya Batticaloa.

Shambulio hilo limefanywa saa chache baada ya serikali kuwalaumu waasi wa Tamil Tigers kwa kufanya shambulio la kujitoa muhanga maisha katika kambi ya jeshi la wanamaji.

Waasi wa Tamil Tigers waliokuwa katika boti waliingia bandari moja na kuivamia kambi ya jeshi la wanamaji la Sri Lanka mjini Galle, mji wa kitalii ulio kusini mwa nchi hiyo. Baharia mmoja na waasi watatu wameuwawa katika uvamizi huo.

Maofisa wa mjini Galle wametangaza marufuku ya kutotembea nje kuzuia maandamano yasitokee. Shambulio la waasi wa Tamil Tigers limefanyika wakati mazungumzo ya kutafuta amani kati ya serikali ya Sri Lanka na waasi hao, yakitarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwezi huu mjini Geneva Uswissi.