CAMP PENDLETON, CARLIFORNIA: Wanajeshi wanane wa Marekani washtakiwa
22 Desemba 2006Waongozaji mashtaka wa jeshi la Marekani wamewafungulia mashtaka wanajeshi wanane kuhusiana na mauaji ya raia 24 ambao hawakuwa na silaha katika mji wa Haditha nchini Irak.
Kanali Stewart Navarre, wa jeshi la Marekani, aliyasoma mashtaka hayo kwenye mkutano na waandishi wa habari huko Camp Pendleton, Carlifornia. Wanajeshi wanne walishtakiwa kwa kutoripoti au kutochunguza vifo vya wairaki hao.
Stewart amesema, ´Kulingana na ripoti ya uchunguzi mashtaka kadhaa yamewasilishwa dhidi ya wanajeshi wanne kuhusu vifo vya wairaki mnamo tarehe 19 Novemba mwaja jana. Pia wanajeshi wanne wanashtakiwa kwa kushindwa kuripoti au kuchunguza vifo vya wairaki. Mashtaka yanajumulisha mauaji, kutojali kazi, udanganyifu na kuzuia haki.´
Wanajeshi hao wanakabiliwa na hukumu ya kifo iwapo watapatikana na hatia. Mauaji ya Haditha yalifanyika mnamo mwezi Novemba mwaka jana. Inakisiwa yalifanywa kulipiza kisasi kuuwawa kwa mwanajeshi wa Marekani katika mlipuko wa bomu lililokuwa limetegwa kando ya barabara.