BAGHDAD: Wapiganaji wa Irak wataka mashambulio ya kulipiza kisasi yafanywe
23 Februari 2007Matangazo
Makundi ya wapiganaji nchini Irak likiwemo kundi la al-Qaeda, yametoa mwito wa kufanywa mashambulio ya kulipiza kisasi kufuatia madai mapya kuhusu ubakaji.
Madai hayo ya pili, dhidi ya kikosi cha usalama cha Irak kilicho na idadi kubwa ya Washia, yalitangazwa hadharani jana.
Kiongozi wa al-Qaeda nchini Irak, Abu Hamza al Muhajir, amewataka wafuasi wake waongeze mashambulio dhidi ya ya vikosi vya usalama vya Irak kulipiza kisasi hujuma hizo za ubakaji mjini Baghdad na mji wa kaskazini wa Tal Afar karibu na mpaka wa Syria.
Wanasiasa wa madhehebu ya Sunni wanaoipinga serikali inayoongozwa na Washia wametumia madai ya ubakaji kusema wanajua mamia ya visa vya aina hiyo ambavyo bado havijatangazwa hadharani.