EU kukamilisha makubaliano ya biashara huria na India
26 Januari 2026
Viongozi wa Umoja wa Ulaya wameungana na viongozi wa India katika gwaride la kuadhimisha siku ya Jamhuri ya India leo. Hafla hiyo inafanyika siku moja kabla ya pande hizo mbili kukamilisha makubaliano ya muda mrefu ya biashara huria.
Rais wa Baraza la Ulaya, Antonio Costa na Rais wa Halmashauri ya Umoja wa Ulaya, Ursula von der Leyen, wanahudhuria hafla hiyo, kabla ya mkutano wa kilele kati ya Umoja wa Ulaya na India utakaofanyika kesho Jumanne, ambapo pande hizo mbili zinatarajiwa kutangaza mkataba muhimu wa biashara huria pamoja na ushirikiano wa kiusalama.
India na Umoja wa Ulaya zimekuwa zikijadiliana juu ya makubaliano ya biashara kwa zaidi ya muongo mmoja kabla ya ushuru wa kibiashara uliowekwa na Rais wa Marekani Donald Trump kuzisukuma pande hizo kuharakisha juhudi zao mwaka jana.