1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump akutana na Kim wa Korea Kaskazini

Zainab Aziz Mhariri:Sudi Mnette
30 Juni 2019

Rais Donald Trump wa Marekani amekutana na kiongozi wa Korea Kaskazini katika eneo lisilo la kijeshi la mpaka wa Korea mbili ambapo viongozi hao wawili walipeana mikono kuonesha ishara ya matumaini ya amani.

https://p.dw.com/p/3LLzv
USA | Nordkorea | Entmilitarisierte Zone | Donald Trump | Kim Jong Un
Picha: Reuters/K. Lamarque

Rais wa Marekani Donald Trump na Kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un wakubaliana kuanzisha tena mazungumzo ya nyuklia yaliyokwama.

Katika wiki zijazo, vikosi kazi vitaanzishwa kutoka pande zote mbili. Upande wa Marekani utaongozwa na Waziri wa Mambo ya nje wa Marekani Mike Pompeo. Trump hakutoa maelezo zaidi kuhusu yake yatakayojadiliwa lakini ameeleza wazi kwamba vikwazo dhidi ya Korea Kaskazini vitaendelea kubaki kwa muda.

Marekani imeitaka Korea Kaskazini isimamishe kabisa mpango wake wa nyuklia. Korea Kusini na Marekani pia wanahimiza upatikane mkataba rasmi wa amani kati ya Korea mbili.

Kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani Papa Francis
Kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani Papa FrancisPicha: picture-alliance/Zumapress/E. Inetti

Kiongozi wa kanisa katoliki duniani Papa Francis amepongezamkutano wa Jumapili kati ya Rais wa Marekani Donald Trump na Kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un, asema ana matumaini kuwa mkutano huo utawezesha kupatikana amani.

Huu ni mkutano wa tatu kwa viongozi hao wawili katika kipindi cha mwaka mmoja. Kukutana kwa viongozi hao kumeongeza matumaini ya kuyarejesha mezani mazungumzo ya nyuklia yaliokwama. Rais Trump aliandamana na Kim kuvuka eneo hilo la mpaka lisilo la kijeshi na ambalo kwa miaka kadhaa limekuwa katika fukuto la Vita Baridi.

Trump ndiye Rais wa kwanza wa Marekani aliye madarakani kukanyaga eneo hilo la upande wa ardhi ya Korea Kaskazini. Baada ya mazungumzo ya takribani dakika 50 Trump na Kim walirejea upande wa Korea Kusini na kuungana na Rais Moon Jae-in kwa mazungumzo mafupi. Baadae Trump na Kim walifanya mazungumzo ya faragha.

Rais Donald Trump alikutana na wanajeshi wa Marekanikatika kambi ya wanahewa ya Osan iliyopo kusini mwa mji mkuu wa Korea Kusini, Seoul. Hatua hiyo ndio ilikamilisha safari yake ya barani Asia na kisha kurudi Washington.

Trump aliwasili Korea Kusini jana jioni kwa ajili ya mazungungumzo na Moon baada ya kuhudhuria mkutano wa kilele wa mataifa 20 yalioendelea kiviwanda duniani huko Osaka, Japan, ambapo alifanya ziara ya kushtukiza na kutoa wito wa kutaka kuonana na kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un.

Vyanzo:/AP/RTRE/p.dw.com/p/3LLcB