Zelensky ayasifu mazungumzo ya kutafuta amani Ukraine
25 Januari 2026
Mazungumzo hayo yamewahusisha wawakilishi kutoka Ukraine, Urusi na Marekani. Zelensky kupitia chaneli yake ya Telegram amesema pande zote katika majadiliano hayo zimekubaliana kuripoti kwa viongozi wao kila kipengele cha mazungumzo na kuratibu hatua zijazo.
Kwa mujibu wa afisa wa Marekani aliyetoa sharti la kutokutajwa jina, awamu ijayo ya mazungumzo itafanyika Februari Mosi.
Jeshi, uchumi vyatawala mazungumzo
Afisa huyo amesema majadiliano yaliyokwisha yalijikita kwenye masuala mapana yanayohusu jeshi na uchumi pamoja na uwezekano wa kupata makubaliano ya kusitisha vita.
Hii ni mara ya kwanza kwa maafisa wa utawala wa Rais Donald Trump kukaa chini kwa mazungumzo na wawakilishi wa Ukraine na Urusi kama sehemu ya juhudi za kuvikomesha vita nchini Ukraine vilivyodumu kwa karibu miaka minne.