1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kanada haiondoshi uwezekano kuingia vitani dhidi ya Iran

5 Machi 2026

Waziri Mkuu wa Kanada, Mark Carney, amesema hawezi kuondosha uwezekano wa nchi yake kushiriki kijeshi dhidi ya Iran kwenye vita vinavyoendelea kwenye eneo la Mashariki ya Kati.

https://p.dw.com/p/59oiR
Kanada Montreal 2026 | Mark Carney
Waziri Mkuu wa Kanada, Mark Carney, anasema licha ya kuwa mashambulizi ya Marekani na Israel dhidi ya Iran yalikuwa ukiukwaji wa sheria za kimataifa, haondowi uwezekano wa nchi yake kujiunga na vita hivyo.Picha: Christinne Muschi/The Canadian Press/ZUMA/picture alliance

Ziara yake ya wiki hii nchini Australia imetandwa na vita hivyo vilivyoanzishwa na Marekani na Israel dhidi ya Iran, hasa baada ya kiongozi huyo wa Kanada kunukuliwa wiki chache nyuma akipingana na kile alichokiita kupasuka kwa "utawala wa dunia unaoelemea upande mmoja."

Akizungumza akiwa na mwenyeji wake, Waziri Mkuu Anthony Albanese mjini Canberra, alisema nchi yake "itasimama na washirika wake na daima itawalinda raia wa Kanada."

Hata hivyo, Carney alikiri kuwa mashambulizi ya Israel na Marekani dhidi ya Iran yalikuwa kinyume na sheria za kimataifa.

Lakini alisema anaunga mkono juhudi za kuizuwia Tehran isiwe na silaha za nyuklia, huku akitowa wito kwa pande zote kuweka silaha chini.