1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAfrika Kusini

Pretoria inajenga ukaribu zaidi na Beijing kuliko Marekani

18 Februari 2026

Afrika Kusini inaimarisha uhusiano wake wa kibiashara na China, ikiungwa mkono na upatikanaji wa bidhaa zisizotozwa ushuru, ahadi za uwekezaji na uhusiano wa kibiashara unaopanuka kwa kasi.

https://p.dw.com/p/58yys
China Ramaphosa na Xi
Rais Ramaphosa akisalimiana na Rais XiPicha: Li Xueren/XinHua/picture alliance

Hadi mwaka 2008, Marekani  ilikuwa mshirika mkuu wa biashara wa Afrika Kusini — kabla ya China kuipiku, na kufikia kiwango cha biashara ya pande mbili cha dola bilioni 52.5 (€ bilioni 44.25) mwaka 2024.

Mkataba wa Sheria ya Ukuaji na Fursa kwa Afrika (AGOA), iliyopitishwa na Bunge la Marekani mwaka wa 2000 kwa lengo la kuimarisha fursa za kiuchumi kwa Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara, ilitoa ufikiaji usiotozwa ushuru kwa soko la Marekani kwa takriban bidhaa 1,800 za Afrika Kusini. Lakini utulivu uliokuwa ukitolewa umetikiswa kabisa.

Mnamo 2025, utawala wa Trump uliweka ushuru wa jumla wa asilimia 30 kwa bidhaa zote zinazoagizwa kutoka Afrika Kusini, hatua ambayo wachambuzi wanaona inapingana na nia ya muswada huo. Mwaka huu, Trump aliurefusha mkataba wa AGOA, hadi Desemba 31, 2026, ikiwa ni muda mfupi zaidi kuliko ulivyorefushwa huko nyuma kwa miaka 15 na 10.

Masharti ambayo hapo awali yaliifanya Marekani kuwa soko la kuaminika sasa yanaonekana kuwa dhaifu na yenye mabadiliko ya kisiasa, na kuisukuma Afrika Kusini kutafuta njia mbadala.

Emmanuel Matambo ni Mkurugenzi wa Utafiti katika Kituo cha Masomo ya Mahusiano ya China na Afrika. "Afrika Kusini inakabiliwa na tatizo katika baadhi ya sekta, lakini si katika sekta vingi. "Unapoangalia takwimu za biashara ambayo Afrika Kusini imekuwa nayo katika miaka 15 iliyopita, hakuna ulinganisho kati ya China na Marekani."

Urusi Kazan 2024 | Vladimir Putin na Cyril Ramaphosa katika mkutano wa kilele wa BRICS
Viongozi wa Jumuiya ya BRICS katika mkutano uliofanyika Urusi 2024Picha: Iranian Presidency/ZUMA/picture alliance

Afrika Kusini inaimarisha uhusiano na China

Umuhimu wa China unaonekana waziwazi. Mnamo 2025, Afrika Kusini ilisafirisha bidhaa zenye thamani ya zaidi ya dola bilioni 13.5 za Marekani kwenda China, hasa madini na vyuma, kulingana na hifadhidata ya Umoja wa Mataifa ya COMTRADE kuhusu biashara ya kimataifa.

China, kwa upande wake, inaongeza ufikiaji wake wa soko barani Afrika. Mnamo 2024, iliondoa ushuru wa forodha kwa bidhaa zinazoagizwa kutoka nchi 33 zilizoendelea barani Afrika na kukuza biashara ya China barani Afrika hadi dola bilioni 296.

Hivi majuzi Afrika Kusini ilisaini Mkataba Mpana wa Ushirikiano wa Kiuchumi, ambao unalenga kutoa ufikiaji usiotozwa ushuru kwa mauzo ya nje ya Afrika Kusini - haswa bidhaa za kilimo - kwa soko kubwa la watumiaji wa China. China iliagiza bidhaa za kilimo zenye thamani ya dola bilioni 207.4 duniani kote mwaka wa 2025.

Mabadiliko haya yanaakisi hatua ya Afrika Kusini ya kupunguza hatari zinazoongezeka zinazohusiana na soko la Marekani. Jumuiya ya wafanyabiashara na wanadiplomasia nchini Afrika Kusini inaonekana kuwa na imani kuhusu mwelekeo wa Rais Cyril Ramaphosa kuelekea Beijing.

Phuti Joyce Tsipa, Balozi Mdogo wa Afrika Kusini mjini Shanghai, China anaeleza "China na Afrika Kusini zina uhusiano mzuri, imara sana. Kwa pamoja tumefikia jumla ya biashara ya pande mbili ya dola bilioni 47.7," "Kuna mengi tunayoweza kuipa China na kuna mengi ambayo China inaweza kuipa Afrika Kusini na Afrika."

China -Rais wa China  Xi akimkaribisha Ramaphosa
Viongozi wa China na Afrika Kusini wakikagua gwaride Picha: Yao Dawei/XinHua/picture alliance

Kwa sasa, China hunufaika na sehemu kubwa ya bidhaa kutoka Afrika Kusini, huku Marekani ikiwa na sehemu ndogo tu. China pia ni muagizaji na mnunuzi mkubwa wa rasilimali za madini nchini Afrika Kusini, ikiwa ni pamoja na dhahabu, madini ya chuma, manganese, na mengineyo.

Swali la ushuru: Je, Afrika Kusini inaweza kuelekeza kwingine mauzo ya nje?

Mahitaji ya China kwa bidhaa za Afrika Kusini ni zaidi madini na malighafi, huku Marekani ikinunua vitu vya thamani kubwa kama vile magari na bidhaa fulani za kilimo. Kwa mfano, magari na vipuri vya magari — bidhaa zinazouzwa nje zaidi nchini Afrika Kusini — havifikii mahitaji ya uagizaji ya China, hasa kwa kuwa sasa China imeipiku Japan kama muuzaji nje mkuu wa magari duniani.

Kwa mtaalamu wa biashara wa China na Afrika, Matambo, sekta za viwanda vya magari na kilimo cha bustani nchini Afrika Kusini zinaweza kukabiliwa na changamoto, kwani zilikuwa ndio ziliongoza kwa mauzo ya kwenda Marekani kabla ya ushuru wa upande mmoja wa Trump.

"Sidhani kama Afrika Kusini iko njiapanda kati ya Marekani na China, hasa linapokuja suala la biashara. Linapokuja suala la siasa, hilo ni suala jingine kabisa."

Afrika Kusini Johannesburg 2023  | Mkutano wa 15 wa BRICS: Viongozi Xi Jinping, Cyril Ramaphosa, Lula da Silva, Narendra Modi na Sergei Lavrov
Viongozi wa BRICS: Lula da Silva, Xi Jinping, Cyril Ramaphosa, Narendra Modi na Sergei LavrovPicha: Li Xueren/Xinhua/picture alliance

Hata hivyo, Matambo alieleza kuwa haitakuwa rahisi kwa Afrika Kusini kuhamishia China baadhi ya bidhaa za nje ilizosafirisha kwenda Marekani.

Mauzo ya nje ya Afrika Kusini kwenda China yanabaki kutawaliwa na malighafi zenye thamani ya chini - madini, vyuma, na bidhaa za kilimo - huku uagizaji kutoka China kimsingi ukiwa bidhaa za viwandani. Kuongeza thamani ndani ya Afrika bado ni muhimu kwa kushughulikia usawa wa kibiashara unaoendelea.

Nafasi ya Afrika Kusini 'inayoyumba' katika AGOA

Wachumi wengi wanakubaliana, ikizingatiwa kwamba AGOA bado inatoa ufikiaji usiotozwa ushuru kwa maelfu ya bidhaa zinazoelekea Marekani. Hata kama baadhi ya bidhaa hizo zitazidiwa na ushuru, Afrika Kusini ina mengi zaidi ya kupoteza kwa kujiondoa kwa hiari katika makubaliano hayo.

"Haitakuwa vyema kwa Afrika Kusini kujiondoa katika AGOA," Matambo alisema. "Hilo litakuwa ni kujikata pua ili kudharau uso wako."

Lakini huku Trump akitishia kuongeza ushuru wa biashara dhidi ya nchi anazoziona kuwa si rafiki kwa sera yake ya "Marekani Kwanza", AGOAinabaki katika hali isiyo imara.

Mnamo 2025, uhusiano wa Marekani na Afrika Kusini ulizorota kutokana na mizozo ya siasa za kikanda inayohusisha BRICS+, vita vya Israel huko Gaza, na madai ya 'mauaji ya halaiki' yaliyofanywa dhidi ya wakulima Wazungu wa Afrika Kusini.

Huku Matambo akisisitiza kwamba Afrika Kusini ina kila haki na wajibu wa kutafuta masoko mbadala, alipendekeza Pretoria iongeze biashara yake ndani ya bara hilo kwanza. Alisema: "Upendo huanzia nyumbani. Afrika kwanza, China, nchi za Asia na kisha Umoja wa Ulaya (EU)."

Takwimu zinaunga mkono madai yake: Mnamo 2025, Afrika iliingiza zaidi ya nusu ya mauzo ya nje ya kilimo ya Afrika Kusini, yenye thamani ya dola bilioni 8, na kulifanya bara hilo kuwa soko kubwa zaidi la bidhaa za kilimo za Afrika Kusini. Kulingana na Matambo, utanuaji wa masoko, — na sio mbadala — ndiyo njia salama zaidi ya kusonga mbele kwa Afrika Kusini.

 

Ruka sehemu inayofuata Gundua zaidi