1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Migogoro

Iran yakanusha kutoa adhabu ya kifo dhidi ya waandamanaji

18 Januari 2026

Msemaji wa idara ya mahakama ya Iran amesema hadi sasa hakuna adhabu yoyote ya kifo iliyotolewa inayohusiana na maandamano ya hivi karibuni ya kuipinga serikali.

https://p.dw.com/p/570w7
Iran imesema haijatoa adhabu ya kifo kufuatia maandamano ya hivi karibuni
Kiongozi wa juu zaidi wa Iran, Ayatollah Ali Khamenei Picha: Iranian Leader Press Office/Anadolu Agency/IMAGO

Afisa huyo amesema mchakato wa kutoa adhabu ya aina hiyo ni mgumu na mrefu unaoweza kuchukua muda wa miezi hadi miaka kadhaa. Aidha, amewatuhumu baadhi ya watu waliohusika na maandamano hayo kuwa ni mamluki wenye uhusiano na mashirika ya ujasusi ya Marekani na Israel ya CIA na Mossad.

Wakati huohuo, Afisa wa Iran aliyeomba kufichwa jina lake amesema mamlaka nchini humo zimethibitisha kuwa watu wasiopungua 5,000 wameuawa katika maandamano ya hivi karibuni. Amebainisha kuwa watu 500 kati ya waliouawa ni maafisa wa usalama.

Takwimu za vifo zatofautiana

Jumamosi, Shirika la kutetea Haki za binadamu la HRANA lenye makao yake Marekani lilisema idadi ya vifo imefikia watu 3,308 wakati visa zaidi ya 4,382 vikifanyiwa tathmini. Shirika hilo limethibitisha pia kuwa zaidi ya watu 24,000 wamekamatwa kutokana na maandamano hayo.

Hata hivyo idadi  hiyo inatofautiana na ile iliyotolewa Jumapili na gazeti la Uingereza la Sunday Times inayosema maandamano hayo yanaweza kuwa yamesababisha vifo 16,500 hadi 18,000. Takwimu hizo zimekusanywa kutoka kwa wahudumu wa afya wa hospitali 8 na idara sita za dharura kote nchini Iran japokuwa idadi kamili haiwezi kuthibitishwa