Dakar: Rais Abdoulaye Wade ni mshindi katika uchaguzi wa urais wa Senegal
28 Februari 2007Dakar:
Kiongozi wa Senegal, Abdoulaye Wade, ameshinda awamu ya pili ya urais wa nchi hiyo. Hii ni kwa mujibu wa matokeo ya uchaguzi ya mwanzo mwanzo. Tarakimu kutoka wilaya 35 za nchi hiyo ya Afrika Magharibi zimempa Rais Wade, mwenye umri wa miaka 80, asilimia 55.7 ya kura zilizopigwa. Moja ya vyama vikubwa vya upinzani, kile cha Kisoshalisti, kilisema kinayabisha matokeo hayo. Inasemekana zaidi ya asilimia 75 ya watu walio na haki ya kupiga kura walikwenda vituoni katika nchi hiyo ambayo wakaazi wake wengi ni Waislamu. Uchaguzi huo ulikwenda kwa amani, lakini ilitajwa kwamba mtu mmoja aliuwawa na 13 walijeruhiwa katika mashambulio mawili yaliofanywa na wapinzani waliokuwa na silaha na ambao walijaribu kufuja upigaji kura katika wilaya ya kusini ya Casamance.