1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Yaliyochambuliwa na wahariri wa Ujerumani hii leo

Oummilkhheir14 Februari 2007

Hukmu ya korti kuu ya katiba na makubaliano ya Beijing -ndio mada kuu magazetini hii leo

https://p.dw.com/p/CHTi

Uchunguzi wa kitabibu kama kweli mtoto ni wake na makubaliano kuhusu mradi wa kinuklea wa Korea ya kaskazini ndizo mada zilizohanikiza magazetini nchini Ujerumani hii leo.

Hata hivyo uchunguzi uliofanywa kichini chini hautaweza kutumiwa kama ushahidi mahakamani.Baada ya hukmu ya korti kuu ya katiba,hivi sasa watunga sheria watabidi wasake njia ili kumuondolea hofu baba,na kupata uhakika baada ya utafiti wa viini vya maisha kufanywa kama kweli mtoto ni wake.Ingawa wqahariri wanasifu uamuzi huo hata hivyo maoni yao yanatofautiana.

STUTTGARTER ZEITUNG linahoji “ingawa ni muhimu kutilia maanani masilahi ya kila upande ,hata hivyo haitakua rahisi kwa wahusika na mivutano itazidi kukua.Idadi ya wanaume watakaotaka kujua,hasa uhusiano unapolega lega au kuvunjika,kama kweli mtoto au watoto ni wao,itazidi kuongezeka, hasa pakiwepo suala la fedha.

General Anzeiger linahisi “Kila mtu ana haki ya kujua,amezaliwa na nani.Ni muhimu kwa kitambulisho cha kila kiumbe,na watoto wa kulea pia wana haki ya kuambiwa wamezaliwa na nani.Anaeitambua haki hiyo hawezi kuwalaumu wanaume wanapotaka kujua kama watoto kweli ni wao.”

Gazeti la NORDBAYERISCHE KURIER linasema “ uchunguzi wa DNA ndio uliowafungulia njia akina baba kuondowa dhana.Lakini haki kamili bado hawana.Ushahidi ni huu ,utafiti uliofanywa kisiri siri,japo unadhihirisha mtoto si wa mtu,hautambuliwi mahakamani.”

Mada nyengine magazetini inahusu makubaliano yaliyofikiwa jana kuhusu mradi wa kinuklea wa Korea ya kaskazini.

“Kumbe inawezekana eti” linaandika gazeti la mjini München-ABDENZEITUNG.Wamerakani wanaweza bado kufanikiwa katika siasa ya nje.Baada ya kizungumkuti cha Irak na Mashariki ya kati,angalao kuna habari za kutia moyo kutoka Korea ya kaskazini.

Frankfurter Allgemeine Zeitung linasema,”Mradi mpaka sasa ni wajumbe wa Korea ya kaskazini tuu mjini Beijing ndio waliounga mkono makubaliano hayo.Kim Jong il hakusema chochote?

NEUE DEUTSCHLAND la mjini Berlin linajiuliza kama kweli haya ndo yale makubaliano yaliyokua yakitarajiwa tangu miaka kadhaa iliyopita kuhusu mradi wa kinuklea wa Korea ya kaskazini.

Gazeti linakumbusha, mara nyingi katika mazungumzo haya ya pande sita mjini Beijing,watu walikua wakishangiria ufanisi,na baadae kujikuta pale pale-hakuna kilichofanikiwa.Lakini labda sasa makubaliano ya kweli yamefikiwa.Korea ya Kaskazini inataka kusitisha mradi wake wa kinuklea ili badala yake ipatiwe misaada ya kiuchumi.Yale yale yaliyopigiwa upatu mwaka 2003-japo kama safari hii makubaliano ni bayana-kwa hivyo si haba.Makubaliano ya Beijing ni hatua muhimu kuelekea usalama barani Asia-Kama matumaini hayo yatakamilika, tusubiri tuone.

Gazeti la NEUEN TAG linahisi kipya hapa ni msimamo wa rais George W.Bush kuelekea Korea ya kaskazini.Hakuna tena vitisho na shinikizo badala yake Marekani na Japan zimeahidi kuendeleza mazungumzo yatakayopelekea kurejeshwa uhusiano wa kawaida na kuanzisha uhusiano wa kibalozi pamoja na Korea ya Kaskazini.