Uchumi wa Ujerumani waimarika
13 Agosti 2010Huo ni ukuaji mkubwa kabisa wa uchumi tangu ulipopatikana muungano wa Ujerumani, Oktoba mwaka 1990. Ukuaji huo umevuka kiwango kilichokadiriwa na wataalamu waliotazamia ukuaji wa asilimia 1.3 tu. Kulinganishwa na mwaka jana, ukuaji katika robo ya pili ya mwaka huu, umeongezeka kwa asilimia 4.1.Kwa sehemu kubwa, uwekezaji imara na mauzo ya nje yaliyoimarika ndio yaliyosaidia ukuaji huo. Baada ya China, Ujerumani ndio muuzaji mkubwa kabisa wa bidhaa katika nchi za nje. Lakini hata matumizi ya watu binafsi na serikali pia yamechangia sehemu yao kuimarisha uchumi wa nchi.
Waziri wa uchumi wa Ujerumani, Rainer Bruederle amesema," baada ya uchumi kudodora katika mwaka 2009, kwa kiwango ambacho hakijawahi kutokea tangu kumalizika kwa vita vikuu vya pili, sasa Ujerumani inashuhudia ukuaji wa babu kubwa." Wakati huo huo akaongezea kuwa, tarakimu za uchumi wa Ujerumani ulioimarika, unadhihirisha kuwa serikali inapaswa kuendelea na mpango wake wa kupunguza nakisi katika bajeti hata kama ukuaji wa kiuchumi utaingiza fedha zaidi serikalini.Hata mwanauchumi Julian Callow wa Barclays Capital, anasema tarakimu hizi mpya zinaonyesha kuwa Ujerumani ipo njiani kupata ukuaji wa kama asilimia tatu au hata zaidi ya hiyo katika mwaka huu wa 2010 - yaani ukuaji wake utakuwa mkubwa kuliko ilivyotabiriwa.
Kwa upande mwingine, Ufaransa ambayo baada ya Ujerumani ni nchi yenye uchumi mkubwa kabisa barani Ulaya, mwaka jana ilishuhudia uchumi wake ukidorora kwa asilimia 2.5. Lakini leo hii, waziri wa uchumi wa Ufaransa, Christine Lagarde amesema, uchumi wa nchi hiyo umekuwa kwa asilimia 0.8 katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita, kulinganishwa na miezi mitatu ya mwanzo ya mwaka huu. Vile vile amesema kuwa nafasi 35,000 mpya za kazi zimezinduliwa katika robo ya pili ya mwaka huu. Hata hivyo aliashiria kuwa hakutokuwepo mabadiliko katika ukuaji wa asilimia 2 na nusu uliyotabiriwa. Serikali ya Rais Nicolas Sarkozy inatazamia ukuaji wa asilimia 1.4 kwa mwaka huu mzima nchini Ufaransa.
Nchi zingine zilizochochea hisia za matumaini ni Uholanzi ambako tarakimu rasmi zimeonyesha kuwa pato la jumla la ndani limeongezeka kwa asilimia 0.9 katika robo ya pili ya mwaka na uchumi wa Austria umekuwa kwa kiwango hicho pia. Nayo, Uhispania iliyojikokota kutoka hali mbaya ya kiuchumi katika robo ya kwanza, kwa ukuaji wa asilimia 0.1, sasa imetoa tarakimu mpya zinazoonyesha kuwa uchumi wake umekua kwa asilimia 0.2 katika robo ya pili ya mwaka huu.
Mwandishi: P.Martin/RTRD/RTRE
Mhariri: Charo,Josephat