1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Miaka 60 tangu Ujerumani iwaalike Waturuki nchini mwao

6 Oktoba 2021

Tarehe 30 mwezi huu wa Oktoba itakuwa ni miaka 60 tangu Ujerumani ilipoingia makubaliano ya kuleta wafanyakazi wa kigeni kutoka Uturuki.

https://p.dw.com/p/41LpL
Symbolbild Jugendliche Deutschland Türkei
Picha: picture-alliance/dpa/D. Karmann

Mkataba huo ulisainiwa baina ya Ujerumani na Uturuki mwaka 1961 na umezifanya mpaka leo nchi hizo mbili kuwa na mahusiano ya muda mrefu. Ripoti hii ya mwandishi wa DW Peter Hille inaangazia kumbukumu ya mkataba huo na changamoto zilizopo mpaka sasa kuelekea Waturuki waishio Ujerumani

Baada ya vitu kuu vya pili vya dunia Ujerumani ilipata maendeleo makubwa sana ya kiuchumi na ilikuwa na upungufu wa wafanyakazi. Moja ya nchi zilizotoa wafanyazi wa kigeni ilikuwa ni Uturuki na mkataba huo ulisainiwa tarehe 30 mwezi wa Oktoba mwaka 1961. Mkataba huo umepelekea watu wengi wenye asili ya Uturuki kuendelea kuishi Ujerumani mpaka leo hii.

Maelfu ya watu walitoka Uturuki kama wafanyakazi wa kigeni na kuja kufanya kazi nchini Ujerumani katika viwanda vilivyokuwa vinakua kwa kasi.

Kuna Waturuki karibu milioni 3 wanaoishi nchini Ujerumani

Ingawa mkataba huo wa wafanyakazi wa kigeni ulitaka wafanyakazi waje na kurudi Uturuki baada ya kipindi fulani, sera hiyo ilibadilika baadaye wakati serikali ya Ujerumani ilipoamua kuwaachia wafanya kazi hao walete familia zao. Familia za wafanyakazi hao zilikuja na wao wakaanzisha maisha mapya nchini Ujerumani.

Hiyo imesababisha mpaka sasa miaka 60 baadaye, Ujerumani kuwa na watu wenye asili ya Uturuki wapatao takribani milioni 3. Burak Yilmaz ni kizazi cha tatu cha wafanya kazi hao wa kigeni, ambaye babu yake alikuja Ujerumani mwaka 1963.

Angela Merkel beim Balkan-EU_Gipfel in Slowenien
Kansela Angerla Merkel wa UjerumaniPicha: Petr David Josek/ASSOCIATED PRESS/picture alliance

Babu yake Yilmaz alisafiri kwa treni kutoka Instanbul mpaka Munich na baadaye kwenda kufanya kazi kaskazini magharibi mwa Ujerumani. Huko alianza kufanya kazi kama mchimba madini na baadaye aliajiriwa katika shirika la reli.

Bibi yake Yilmaz alifanya kazi katika kiwanda cha kutengeneza chakula na kipindi hicho walikuwa wanafanya kazi siku nzima wakati watoto wao wakiwa shuleni. Yilmiz anasema kwamba walichotaka babu na bibi yake ni kwamba watoto wao wawe na maisha mazuri.

Yeye mwenyewe Yilmiz amezaliwa mwaka 1987 katika mji wa Duisburg uliopo magharibi mwa Ujerumani. Akivuta picha ya wakati huo alipokuwa mdogo, anakumbuka jinsi wenzake walivyokuwa wanamwona mgeni na mwenye matatizo.

Ingawa yeye amezaliwa hapa, lakini katika macho ya wajerumani alikuwa anaonekana kama mgeni. Sasa Yilmiz ni mwandishi wa vitabu na muelimishaji na amejidhatiti sana katika mada zinazohusu maana ya neno nyumbani. Kwa upande wake nyumbani inamaanisha nyumba nyingi kwa maana ya kwamba yeye ni Mjerumani, Mturuki na MKurdishi.

Yilmiz anaamini kwamba bado nchini Ujerumani kuna tatitizo la ubaguzi wa rangi na kwa mara ya mwisho amepitia tukio hilo la ubaguzi siku ya tarehe 26 mwezi wa tisa wakati wa uchaguzi wa Ujerumani. Mchunguza vitambulisho vya wapiga kura alikiangalia kitambulisho chake kwa makini huku akiwa na wasiwasi kama kweli Yilmiz ni mjerumani.

Kizazi cha Waturuki kimeweza kupanda kielimu

Yilmiz anadai kwamba bado nchini Ujerumani kuna watu ambao wanaamini kwamba wajerumani ni wale wenye macho ya bluu na nywele nyeupe za kizungu.

Haci-Halili Uslucan ambaye ni mkuu wa Taasis ya utafiti katika mada za Uturuki na uhamiaji katika chou kikuu cha Essen-Duisburg anasema katika katika kila waturuki 10 kuna wanane ambao wanapitia ubaguzi kila mwaka.

Putin empfängt Erdogan in Sotschi
Rais Reccep Tayyip Erdogan wa UturukiPicha: Vladimir Smirnov/Sputnik/REUTERS

Uslucan anaamini kwamba kati ya sekta zinazohitaji sana maendeleo ni kwenye upande wa elimu. Kizazi cha kwanza cha wafanyakazi kutoka Uturuki kilikuwa na kiwango cha elimu ya shule ya msingi tu. Vizazi vyao vilivyofuata viliweza kufika mpaka darasa la kumi.

Kizazi cha tatu na cha nne kimeweza kupanda kielimu na kufikia secondari ya juu. Mpaka sasa bado kuna utofauti kidogo wa kufikia ngazi ya juu ya sekondari, kwani bado walimu wengi wa Ujerumani hawawapi ripoti nzuri watu wenye asili ya Uturuki ili waweze kufika sekondari ya juu na chuo kikuu.

Yilmaz mwenyewe anakumbuka jinsi mwalimu wake alivyokuwa na wasiwasi wa kumpa mapendekezo mazuri ya kumwezesha kuendelea zaidi kimasomo.

Kwa sasa watu kama Yilmaz na waturuki wengine wana utambulisho wa aina yao nchini Ujerumani na wanajiamini. Ingawa kumekuwa na changamoto za kibaguzi na kupata elimu, sasa wanataka majukumu zaidi na kuchangia kwenye jamii.

Miaka hiyo 60 ya tokea mababu zao walipofika kufanya kazi na wao kuzaliwa nchini Ujerumani, inafanya waone Ujerumani ni nchi yao pia.