1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Merkel asema ataunga mkono Uingereza kujitoa EU

Sekione Kitojo
21 Novemba 2018

Ujerumani itaunga mkono makubaliano ya Brexit siku ya Jumapili, na kutumai kwamba pingamizi la Uhispania kuhusiana na maelezo  kuhusu mzozo wa ardhi  ya Uingereza  ya Gibraltar unaweza kutatuliwa ifikapo wakati huo.

https://p.dw.com/p/38fZi
Deutschland Bundeskanzlerin Angela Merkel im Bundestag
Picha: picture-alliance/dpa/M. Kappeler

 Amesema  hayo  kansela  wa  Ujerumani Angela  Merkel  alipokuwa  akihutubia  bunge  leo  mchana mjini  Berlin. Pia  ametupilia  mbali  miito  kutoka  kwa wabunge wenye  siasa  kali  za  mrengo  wa  kulia  kuacha kuunga  mkono  makubaliano  yanayoungwa  mkono  na Umoja  wa  mataifa  kuhusu  uhamiaji.

Deutschland Bundeskanzlerin Angela Merkel im Bundestag
Kansela wa Ujerumani Angela MerkelPicha: picture-alliance/dpa/M. Kappeler

Waziri  mkuu  wa  Uhispania  Pedro Sanchez  amesema jana  kwamba  serikali  yake  itapiga  kura  dhidi  ya mswada  wa  Umoja  wa  Ulaya  kuhusu  makubaliano  ya Uingereza  kujitoa  kutoka  Umoja  huo  yaani  Brexit  iwapo maelezo  yaliyomo  katika  mswada  huo kuhusu  Gibraltar hayatabadilishwa. Gibraltar  inatarajiwa  kujitoa  kutoka Umoja  wa  Ulaya  pamoja  na  Uingereza  ifikapo  mwezi Machi, licha  ya  kuwa  asilimia  96  ya  wakaazi  wake walipiga  kura  katika  kura  ya  maoni  mwaka  2016  nchini Uingereza  kubakia  katika  kundi  hilo  la  mataifa.

"Tunafahamu ni  vigumu  kiasi  gani  majadiliano  haya yalivyo  nchini  Uingereza, lakini naweza  kusema  kwa Ujerumani  kwamba  tutakubaliana  na  makubaliano  ya kujitoa," Merkel  aliwaambia  wabunge  leo  Jumatano wakati  wa  mjadala  wa  bajeti.

"Bado tunapingamizi  kutoka  Uhispania. Siwezi  kusema kwa  hakika  vipi tunaweza  kutatua suala  hili, lakini nina matumaini  litatatuliwa  siku  ya  Jumapili. Katika  siku zinazokuja kazi  zaidi  itafanyika  kuhusiana  na  uhusiano wa  hapo  baadaye  kati  ya  Uingereza  na  Umoja  wa Ulaya."

Deutschland Bundeskanzlerin Angela Merkel im Bundestag
Wabunge wakimsikiliza kansela Merkel bungeni mjini BerlinPicha: picture-alliance/dpa/R. Hirschberger

Ushirikiano  mzuri  na Uingereza

Merkel  amesema  katika  hotuba  yake  kwamba   nchi yake  inataka  kujenga  ushirikiano  mzuri  na  Uingereza baada  ya  Brexit. Katika  hotuba  yake  amesisitiza kwamba  yeye  pamoja  na  serikali  yake  watafanya  kila linalowezekana  kuhakikisha  hilo  linawezekana.

Pia Merkel  alipuuzia  miito  kutoka  kwa  wabunge  wa vyama  vya  siasa  kali  za  mrengo  wa  kulia kwamba Ujerumani  iondoe uungaji  wake  mkono  kwa makubaliano  ya Umoja  wa  Mataifa  kuhusu  uhamiaji.

AfD Europawahlversammlung
Kiongozi wa chama cha AfD Alexander GaulandPicha: picture alliance/dpa/M. Kappeler

Nchi  kadhaa  ikiwa  ni  pamoja  na  Marekani, Hungary, Austria, Israel, Australia  na  Poland, zimetangaza kwamba  hazitaunga  mkono Mkataba  wa  dunia  wa uhamiaji  salama, utaratibu  mzuri na  wenye kuratibiwa, ambao umepangwa  kuidhinishwa  mwezi  ujao  mjini Marrakech , nchini  Morocco.

Upinzani  umekuja  hususan  kutoka  chama  cha  siasa kali  za  mrengo  wa  kulia  chama  mbadala  kwa Ujerumani AfD, lakini  wabunge  kadhaa  kutoka  chama cha  Merkel pia  wameanza  kuhoji makubaliano  hayo. Merkel  amesema.

"Mkataba  huu kwa  wahamiaji pamoja  na  wakimbizi ndio jibu  sahihi  wakati  tukiwa  mwanzoni  mwa  kutatua matatizo  ya  dunia  kwa  pamoja  kimataifa."

Waziri  wa  afya Jens Spahn ametoa  wito  hivi  karibuni  wa mjadala  mpana  kuhusu  mkataba  huo, iwapo inahitajika, ucheleweshwe ili  kuweza  kuufanya  bora  zaidi.

Jens Spahn
Waziri wa afya wa Ujerumani Jens SpahnPicha: picture-alliance/dpa/F. Gambarini

Akiwasilisha  mswada  wa  bajeti wa serikali  yake  wa euro bilioni 356 kwa  mwaka  2019, Merkel ameelezea  mipango ya  kuwekeza  zaidi katika  huduma ya afya  kwa  watoto na wazee, kuchukua  hatua  za  kuimarisha  ujumuisho  kwa wahamiaji, kupandisha  viwango  vya  malipo  ya  uzeeni na kuimarisha nishati endelevu.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / ape / rtre / dpae

Mhariri: Idd Ssessanga