1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani yasifu operesheni yake nchini Iran

Bakari Ubena (dpa, ap, reuters, afp)
6 Machi 2026

Marekani imesifu operesheni yake nchini Iran na kusema inaelekea kumuangamiza adui hata kabla ya wakati huku ikisisitiza kuwa uwezo wa mashambulizi wa Iran umepungua maradufu ukilinganisha na siku ya kwanza ya vita.

https://p.dw.com/p/59wYU
Teheran | Mashambulizi ya Israel na Marekani katikati ya mji mkuu wa Iran
Mashambulizi ya Israel na Marekani katikati ya mji mkuu wa Iran, TehranPicha: Atta Kenare/AFP

Kamanda mkuu wa Jeshi la Marekani Brad Cooper, amesema mashambulizi ya Iran iwe ya makombora ya masafa marefu au droni yamepungua maradufu ukilinganisha na siku ya kwanza ya mzozo huo wa  Mashariki ya Kati , lakini akasisitiza kuwa wataendelea kuwa makini wakati wote.

Ama Rais wa Marekani Donald Trump kwa upande wake amesifu ufanisi wa operesheni hiyo akisema kuwa jeshi la Marekani, pamoja na washirika wazuri wa Israel, linaendelea kumuangamiza kabisa adui ambaye ni Iran, hata kabla ya muda uliopangwa.

" Pia tunawasihi wanadiplomasia wa Iran kote ulimwenguni kuomba hifadhi na kutusaidia kuijenga Iran mpya, iliyo bora na yenye uwezo mkubwa. Nadhani sasa unaanza mustakabali mzuri zaidi kwa Iran. Na Marekani itahakikisha kwamba kiongozi ajaye wa Iran hatatishia Marekani, Israel, majirani zake au mtu yeyote," alisisitiza Trump.

Umati mkubwa wa raia wa Iran ulikusanyika katikati mwa mji mkuu Tehran kwa ajili ya sala ya kwanza ya Ijumaa tangu kuanza kwa vita hivyo.
Umati mkubwa wa raia wa Iran ulikusanyika katikati mwa mji mkuu Tehran kwa ajili ya sala ya kwanza ya Ijumaa tangu kuanza kwa vita hivyo.Picha: AFP

Aidha, licha ya mashambulizi ya Israel na Marekani kuendelea, umati mkubwa wa raia wa Iran ulikusanyika katikati mwa mji mkuu Tehran na katika maeneo mengine kwa ajili ya sala ya kwanza ya Ijumaa tangu kuanza kwa vita hivyo. 

Picha zilizosambazwa mtandaoni na vyombo vya habari vya Iran zimeonyesha umati wa watu waliovalia nguo nyeusi huku baadhi wakiwa wamebeba bendera za Iran, wakimiminika nje ya Msikiti Mkuu wa Imam Khomeini  mjini Tehran  kwa ajili ya sala ya Ijumaa ambayo pia ni ya kwanza tangu kuuawa kwa kiongozi mkuu wa nchi hiyo Ayatollah Ali Khamenei kufuatia mashambulizi ya Marekani na Israel ambayo yameendelea kwa kasi katika siku hii ya saba ya mzozo huo.

Iran yaendelea kuvurumisha makombora na droni

Iran nayo imeendelea kuishambulia Israel na mataifa jirani ya Ghuba ambako kunapatikana kambi na wanajeshi wa Marekani. Qatar imesema hivi leo kuwa vikosi vyake vya majini havikujeruhiwa licha ya kuwepo ndani ya majengo ya makazi na hoteli yaliyolengwa na Iran huko Bahrain huku Saudi Arabia ikitangaza kudungua droni kadhaa karibu na mji wa Riyadh.

Msemaji wa UNHCR Ravina Shamdasani
Msemaji wa UNHCR Ravina ShamdasaniPicha: Fatih Erel/AA/picture alliance

Katika tukio jingine, Umoja wa Mataifa umeitaka Marekani kuchunguza haraka tukio la shambulizi katika shule nchini Iran ambapo uchunguzi wa gazeti la New York Times unasema huenda shambulio hilo lililosababisha vifo vya wanafunzi zaidi ya 150 lilifanywa na Marekani.

Israel imeendeleza pia mashambulizi yake nchini Lebanon ikidai yanalenga kulidhoofisha kundi la Hezbollah linaloungwa mkono na Iran. Lakini Umoja wa Mataifa umehimiza hivi leo kufanyike uchunguzi wa haraka kuhusu mashambulizi mabaya ya Israel nchini Lebanon, ili kubaini ikiwa yanafanyika kulingana na sheria za kimataifa.

Aidha, Shirika la wakimbizi la  Umoja wa Mataifa  limesema hivi leo kuwa karibu watu 100,000 wameyakimbia makazi yao ndani ya Lebanon ikiwa ni pamoja na maelfu ya wakimbizi wa Syria. Msemaji wa UNHCR Ravina Shamdasani ameielezea hali katika eneo hilo kuwa dharura kubwa ya kibinadamu na kwamba raia ndio wanaolipia gharama kubwa.