1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mafunzo kwa njia ya elektroniki Afrika

Mohamed Dahman3 Juni 2007

Dhima za teknolojia za habari na mawasiliano katika kuboresha elimu barani kote Afrika zimepata nadhari hivi karibuni katika Mkutano wa Kujifunza kwa njia ya Elektroniki barani Afrika.

https://p.dw.com/p/CHki
Watoto wa Kiafrika katika mafunzo kwenye mtandao.
Watoto wa Kiafrika katika mafunzo kwenye mtandao.Picha: picture-alliance/dpa

Elimu ya aina hiyo imezingatiwa katika mkutano wa kila mwaka uliofanyika mwishoni mwa mwezi wa Mei katika mji mkuu wa Kenya Nairobi na kuhudhuriwa na washiriki kutoka duniani kote.

Kujifunzia kwa njia ya Elektroniki kunathibitisha kuwa na manufaa katika sehemu kadhaa za bara la Afrika ambapo kuna uhaba wa walimu wenye ujuzi.

Nchi ya kupigiwa mfano ni Ethiopia.

Ni zaidi ya nusu ya walimu wa nchi hii ya Afrika Mashariki hawana ujuzi jambo ambalo limeifanya serikali kuanzisha mradi wa kujifunza kwa njia ya elektroniki hapo mwaka 2003 anasema hayo Demissew Bekele mkuu wa kitengo cha Teknolojia ya Habari na Mawasiliano ICT katika Wizara ya Elimu.

Tokea wakati huo Ethiopia imewekeza kwa takriban wasimamizi 16,700 kwa mafunzo kwenye vioo vya kompyuta juu ya masomo mbali mbali kwa walimu wanaohitaji msaada kwa kuwapatia mafunzo hayo halikadhalika kwa wanafunzi. Wasimamizi hao wamesambazwa kwa shule zote 775 za sekondari mpango kama huu pia unatarajiwa kutekelezwa kwenye shule za msingi.

Katika nchi jirani ya Kenya kujifunza kwa njia ya elektroniki pia kumeanza kutekelezwa kutokana na mradi wa mfano wa kujifunza kwa njia ya elektroniki mashuleni ambao kwa mara ya kwanza ulitangazwa na NEPAD Ushirikiano Mpya kwa Maendeleo ya Afrika hapo mwaka 2003.NEPAD inataka kuvutia misaada zaidi na msamaha wa madeni kwa Afrika na kuanzishwa kwa masharti mazuri ya kibiashara kwa kuboresha tawala bora katika nchi za Kiafrika.

Shule sita za sekondari nchini Kenya tayari zimeunganishwa na mtandao chini ya juhudi hizo kwa mujibu wa Mary Mmayi afisa wa ushirikiano kwa mradi huo nchini humo.

Ameliambia shirika la habari la IPS kwamba bado wangalipo katika hatua ya maonyesho ambapo baada ya kuunganisha teknolojia ya habari na mawasiliano ICT na kujifunza kwa njia ya elektoniki wataanzisha vituo vya kujifunza kwa njia ya elektroniki vya viwango bora kabisa ambapo wasioweza kujipatia elimu ya sekondari watakuwa wanaweza kujiorodhesha.

Nchini Kenya kuna mipango ya kuongeza kujifunza kwa njia ya elektroniki kwa shule nyengine 122.

Mbali na Kenya nchi nyegine 15 za Afrika zinashiriki katika mradi huo wa NEPAD ambao pia unakusudia kutowa vifaa vya kufundisha na mafunzo kama sehemu ya faida zake.

Hata hivyo baadhi ya walimu wana wasi wasi kwamba mafunzo hayo kwa njia ya elektroniki yumkini hatimae yakawapoteza nafasi zao za ajira kwamba teknolojia hiyo itachukuwa nafasi yao.

Suala la umeme ni muhimu sana katika kufanikisha elimu hiyo kwani huwezi kuingia katika mtandao bila ya umeme.Waziri wa Elimu wa Kenya George Saitoti amesema wizara yake kwa kushirikiana na wizara ya nishati wako katika mradi utakaozipatia umeme shule zote za serikali zilioko vijijini.

Kwa upande wake Rwanda inaangalia uwezekano wa kutumia nishati ya jua kusambaza umeme shuleni nchi hiyo ya Afrika ya Kati pia inashiriki katika mradi wa NEPAD wa mafunzo kwa njia ya elektroniki shuleni.

Ziada ya hilo inajaribu kuwapatia wanafunzi wote ujuzi wa teknolojia ya habari na mawasiliano ambapo karibu shule 2,000 za msingi zimepatiwa kompyuta mbili kwa kila shule na wakati shule 500 za sekondari zimepatiwa kompyuta 10 kwa kila shule.