1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

110810 Nachhaltigkeit contra Wachstum

Zhang,Danhong/DW Wirtschaft16 Agosti 2010

Wataalamu wa uchumi wanatathmini uwezekano wa kutokea msukosuko mpya wa kiuchumi baada ya taarifa kutolewa kwamba uchumi wa Ujerumani umekua kwa kasi kubwa tangu muungano wa Ujerumani

https://p.dw.com/p/OoXA
Michael Müller, aliyekuwa waziri wa mazingira wa UjerumaniPicha: picture-alliance/ dpa/dpaweb

Wataalamu wa uchumi wa Ujerumani wana kuna vichwa ili kutambua iwapo ustawi uliopo sasa utadumu ama pana hatari ya kutokea mdororo mwingine wa uchumi. Wataalamu wengine wanaweka mkazo katika uchumi endelevu kwa maana ya kuepusha upondaji wa raslimali.

Mjadala huo umekuwa unaendelea kwa miaka zaidi ya thelathini nchini Ujerumani. Na sasa unatiwa msukumo mpya. Sababu ni kwamba mgogoro wa uchumi wa hivi karibuni na mabadiliko ya hali ya hewa yemewafanya watu wawe na mashaka juu mfumo wa uchumi wa hadi sasa unaoweka mkazo katika ustawi tu. Mfumo huo wa uchumi unatiliwa mashaka katika namna ambayo haijawahi kutokea.

Aliyeanzisha mjadala huo ni Profesa Gerhard Scherhorn kutoka Mannheim. Profesa huyo amebaini tatizo kuu linalomkabili mwanadamu ni ubadhirifu wa raslimali.

Profesa huyo amesema binadamu wanafanya ubadhirifu wa maliasilia kutokana na kuvuka mipaka katika kuvua samaki hadi kufikia kiwango cha kuwamaliza, kufua maji hadi kupunguza akiba ya msingi na kuteketeza uhai anuai.

Huo pia ndio mtazamo wa aliyekuwa naibu waziri wa wizara ya mazingira ya Ujerumani Michael Müller.

Hapa panahusu, kwamba sasa tumeshapita katika kipindi cha historia ya maendeleo ya viwanda, ambapo kusema kweli tulifuja raslimali za dunia na maisha yetu.

Hakuna mahala ambapo ubadhirifu wa raslimali unaonekana dhahiri kuliko katika nchi inayojulikana kuwa ni muujiza wa kiuchumi, yaani China.

Zaidi ya aslimia 80 ya mito imechafuka. Kati ya miji 20 iliyochafuliwa kwa kiwango kikubwa, 16 ipo nchini China. Ni kweli kwamba katika kipindi cha miaka 30 China imekuwa inafikia ustawi wa karibu asilimia 10 kila mwaka, lakini asilimia tano hadi saba ya ustawi huo unaathirika na kuharibika kwa mazingira.

Juu ya hayo aliyekuwa naibu waziri wa ulinzi wa mazingira wa Ujerumani Michael Müller anaeleza.

"Kwa mfano nikiangalia uchunguzi wa baraza la hali ya hewa duniani, naweza kusema kwamba hasa maeneo ya viwanda karibu na mito yanatishiwa kuwa na ongezeko kubwa la joto. Maana yake ni kwamba China itapaswa kugharamia mpango mkubwa sana wa kuwahamisha watu. Sina uhakika iwapo nchi hiyo inao uwezo huo. Lakini kwa namna yoyote ile ambavyo mtu atatathmini, hayo yatakuwa maafa kwa binadamu."

Naibu waziri huyo amesema dunia imeshafika kwenye mpaka wa ustawi. Lazima paweko na ujenzi mpya wa ikolojia. Hayo ameyasema pia Hans Diefenbacher mtaalamu wa masuala ya uchumi kutoka Heidelberg. Amesema ujenzi mpya wa ikoloja unaweza kuanza mara moja.

Mtaalamu huyo ametoa wito kwa watu wote wa kuwa na ukadirifu na kuwa na moyo wa kutosheka. Lakini kubadili mwenendo wa maisha kunaweza kuathiri pato jumla la ndani ya nchi, kwani linaweza kunywea, wakati wanasiasa wanaweka mkazo katika kulistawisha pato hilo.

Mtaalamu Hans Diefenbacher ameshauri kuliondoa pato la ndani kama kipimo cha ustawi na badala yake kuweka kipimo kipya cha kuonyesha hali ya maisha. Hayo hayazingatiwi katika pato jumla la ndani.

Ameeleza kuwa pato jumla la ndani pia halizingatii namna mapato yanavyogawanywa. Kwa usemi mwingine mgawanyo wa mapato na matumizi ya raslimali yajumuishwe katika kipimo kipya.

Mwandishi/ Zhang,Danhong/DW Wirtschaft/

Tafsiri/Mtullya Abdu

Mhariri/Josephat Charo