1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Human Rights Watch yatahadharisha hali ya kisiasa nchini Zimbabwe.

Scholastica Mazula9 Juni 2008

Shirika la Kimataifa la kutetea haki za Binadamu la Human Rights Watch, limeonya kuwa kuongezeka kwa machafuko ya Kisiasa nchini Zimbabwe, kumezidi kupunguza matumaini.

https://p.dw.com/p/EGTQ
Kiongozi wa chama cha MDC; Morgan Tsvangirai,Na rais wa Zimbabwe Robert Mugabe, kulia.Picha: AP

Limesema kuwa matumaini ya kufanyika kwa uchaguzi wa uhuru na haki yanazidi kupotea nchini humo.

Mkurugenzi wa Human Rights Watch,upande wa Afrika, Georgette Gagnon, amesema tangu kutangazwa kufanyika kwa duru ya pili ya Uchaguzi nchini Zimbabwe, hali ya machafuko imekuwa ikiongezeka zaidi na zaidi.

Kauli hii ya Human Rights Watch, imekuja kufuatia ripoti iliyotolewa ikionyesha ongezeko la vitendo vya utekaji nyara, kupigwa, kuteswa na kuuawa kwa wafuasi wa chama kikuu cha upinzani nchini humo cha Movement for Democratic Change-MDC.

Bwana, Gagnon, amenukuliwa na Shirika la habari la Ufaransa akisema kwamba, Wazimbabwe hawawezi kufanya uchaguzi kwa uhuru, kwa sababu ya kuhofia kuwa huwenda kitendo cha kupiga kura kinaweza kuwasababishia kifo.

Shirika hilo lenye makao yake makuu mjini New York, limesema kuwa hadi sasa limesha orodhesha vifo vya watu thelathini na sita waliouawa kutokana na masuala ya kisiasa na wengine elfu mbili wameathirika na machafuko hayo tangu kufanyika kwa awamu ya kwanza ya Uchaguzi mwezi Machi mwaka huu.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, Chama tawala cha Rais Robert Mugabe wa nchi hiyo, kimekuwa kikiendeleza kampeni za kisiasa za kuendeleza vurugu ikiwa ni pamoja na kuiba, kuharibu au kubomoa, kuchinja wanyama, kuiba vyakula na mali pamoja na kuchoma Moto nyumba za watu wanao kipinga chama hicho.

Human Rights Watch, imesema kuwa kwa bahati mbaya zaidi, hata viongozi wa juu wa jeshi na polisi wamekuwa wakikutikana kujihusisha moja kwa moja katika vurugu hizo.

Ripoti ya Shirika hiyo imeeleza kuwa, Chama cha ZANU-PF, pamoja na washirika wake wametengeneza kambi za kuwatesea watu na wemeandaa mkutano utakao azimia kufanya kampeni kwa wafuasi wa chama cha MDC, ili wafuasi hao wakipigie kura chama cha ZANU-PF, katika duru ya pili ya Uchaguzi.

Makundi ya haki za binadamu yametoa wito kwa Umoja wa Afrika-AU, na Jumuia ya maendeleo ya Kusini mwa Afrika, kusisitiza siasa zenye utulivu na pia kuwachukulia hatua wale wote waliojihusisha na vurugu nchini Zimbabwe.

Bwana Gagnon, amesema Viongozi wa AU na SADC, hawapaswi kukaa nyuma na kuziba macho yao kana kwamba hawajui matatizo yaliyoko nchini Zimbabwe.

Amesema wanapaswa pia kuisafisha Zimbabwe kwakusimamia uchaguzi wote na matokeo, ama Serikali ichukue hatua za haraka za kumaliza machafuko na vitendo vingine vya udhalilishaji.

Katika Uchaguzi wa kwanza uliofanyika Mwezi Mei mwaka huu, Rais Robert Mugabe pamoja na Kiongozi wa chama cha MDC, Morgan Tsvangirai walipata kura sawa baada ya Tume ya Uchaguzi ya Nchi hiyo kutangaza matokeo ya awamu ya kwanza ya uchaguzi ambapo kwa mara ya kwanza chama tawala cha ZANU-PF, kilijikuta kikipoteza wingi wa viti Bungeni.