1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Corona: Maambukizi yaongezeka Ujerumani na Ufaransa

Deo Kaji Makomba Mhariri : Iddi Ssessanga
20 Agosti 2020

Wasiwasi unaongezeka kwamba virusi vya Corona vinaweza kuenea upya barani Ulaya wakati watu wakirejea kutoka likizoni na watoto kurudi shule.

https://p.dw.com/p/3hG6b
Ärzte ohne Grenzen Flüchtlingslager Moria Coronavirus
Picha: MSF/Anna Pantelia

Nchini Marekani, afisa mkuu wa magonjwa ya kuambukiza, Anthony Fauci, alisema serikali haitafanya chanjo ya baadae ya COVID-19 kuwa ya laazima kwa umma. Lakini alisema mamlaka za majimbo zinaweza kuifanya kuwa ya laazima kwa baadhi ya makundi, kama vile watoto.

"Hautaki kuamuru na kujaribu na kumlazimisha mtu yeyote kuchukua chanjo. Hatujawahi kufanya hivyo," Fauci, mjumbe wa kikosi kazi cha White House, alisema wakati wa mazungumzo ya video Jumatano, yalioandaliwa na Chuo Kikuu cha George Washington.

Matamshi yake yalikuja masaa kadhaa baada ya Waziri Mkuu wa Australia, Scott Morrison kutangaza kwamba chanjo ya cvirusi vya Corona, pindi itakapopitishwa, itakuwa ya lazima kwa kila mtu katika nchi yake isipokuwa kwa wale wenye sababu za kitabibu.

Mjadala wa maadili na usalama unaendelea duniani wakati ambapo mbio za kutengeneza chanjo zinakusanya kasi.

Kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani, Papa Francis alisema Jumatano kwamba ugonjwa huo unazidisha usawa kati ya matajiri na masikini, na alitaka chanjo za ulimwengu wote ambazo hazihifadhiwi tu kwa matajiri.

Kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani Papa Francis
Kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani Papa FrancisPicha: picture-alliance/ZUMAPRESS/G. Ciccia

Serikali zingine zimeshikilia mikataba na kampuni, zinatarajia kupata chanjo za kipekee wakati zinatengenezwa kwa matumaini ya kumaliza janga hilo, ambalo sasa limewaua zaidi ya watu 780,000 na kuambukiza zaidi ya milioni 22, kulingana na shirika la AFP.

Ujerumani Alhamisi iliripoti visa vipya 1,707 vya ugonjwa huo katika muda wa saa 24, idadi kubwa zaidi ya kila siku tangu kilele cha janga hilo mwezi Aprili. Nchi imekuwa bora zaidi kuliko majirani wengi wa Ulaya katika kupambana na virusi hivi lakini kama mahali pengine, idadi ya visa imeongezeka sana wakati wa likizo ya majira ya joto.

Ongezeko hilo la maambukizi limelaumiwa kwa watu kurejea likizo kama vile vyama na mikusanyiko ya familia. Shule tayari zilianza tena wiki iliyopita katika sehemu za Ujerumani.

Katika kukabiliwa na ongezeko la visa vya virusi hivyo, Ujerumani mapema mwezi huu ilianzisha vipimo vya bure, vya lazima kwa mtu yeyote anayerudi kutoka maeneo yaliyoonekana kuwa katika hatari kubwa ya maambukizo ya COVID-19.

Naye Kansela Angela Merkel alionya wiki hii ya kwamba hakuwezi kuwa na kulegezwa tena kwa vizuizi vya virus vya Corona. Ufaransa siku ya Jumatano ilirekodi visa vipya za virus vya Corona kwa kiwango cha haraka sana cha kila siku tangu mwezi Mei.

Karibu maambukizi 3,800 ya COVID-19 yalithibitishwa katika masaa 24, kwa mujibu wa kitengo cha DGS cha wizara ya afya, ambacho kilisema "viashiria vyote vinaendelea kupanda na maambukizi ya virusi yanazidi." Siku ya Jumatano Toulouse  ilikuwa ni jiji la kwanza la Ufaransa kutangaza kuwa ni lazima kuvaa barakoa ya uso kwa mtu anapokuwa nje.

Kuvaa barakoa tayari ni lazima kwa usafiri wa umma nchini Ufaransa na ndani ya maeneo ya umma, huku kukiwa na hofu kwamba mzunguko mkubwa wa watu wakati ambapo mapumziko ya majira ya joto yakikaribia mwisho, utasababisha kupanda kwa maambukizi.

Chanzo:/AFP