Watu zaidi wanahofiwa watakufa.
13 Mei 2008Watu wasiopungua 12,000 wamekufa kutokana na tetemeko la ardhi, katika jimbo la Sechuan kusini mashariki mwa China. Na habari zinasema hali ni mbaya zaidi kuliko ilivyofikiriwa hapo awali.
Siku moja baada ya tetemeko hilo kutokea idadi ya watu waliokufa imeshafikia 12,000. Na maiti zaidi zinaendelea kupatikana. Shirika la habari la China Xinhua limesema maalfu wengine wamejeruhiwa katika jimbo la Sechuan kusini mashariki mwa China.
Maafisa wa serikali wamesema wanahofia watu wengi zaidi watakufa kutokana na athari za tetemeko hilo lililokuja na nguvu ambazo hazijawahi kuonekana katika kipindi cha miaka 30 iliyopita nchini China.
Waziri mkuu wa China bwana Wen Jiabao alielitembela jimbo la maafa la Sechuan amesema hali ni mbaya zaidi kuliko ilivyohofiwa hapo awali.
Kitovu cha tetemeko hilo lililofikia nguvu ya 7.8 kilikuwa Chengdu, mji mkuu wa jimbo la Sechuan.
Nguvu ya tetemeko hilo ilifikia hadi miji ya Beijing na hata nje ya China katika mji mkuu wa Thailand, Bhangkok.
Timu ya waokoaji ya wanajeshia na madaktari imewasili katika mji wa Wenchua ambao umekatika kimasiliano na miji mingine,kutokana na nguvu ya tetemeko.
Lakini habari zinasema juhudi za kuwakoa watu zaidi zinakabiliwa na ugumu kutokana na mvua kubwa na kutokana na barabara kuharibika sana.