1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waziri wa Ujerumani Baerbock ziarani Ukraine

21 Mei 2024

Waziri wa mashauri ya kigeni wa Ujerumani Annalena Baerbock leo amekitembelea moja ya kituo kikubwa cha kufua umeme nchini Ukraine.

https://p.dw.com/p/4g6AY
Baerbock zu Solidaritätsbesuch in Ukraine
Picha: Jörg Blank/dpa/picture alliance

Kituo hicho kiliharibiwa na makombora ya Urusi na baerbock amepewa taarifa kuhusu athari za shambulizi hilo kwa ugavi wa nishati wa Ukraine.

Baerbock amewasili mjini Kyiv katika hatua ya kuonyesha mshikamano kwa Ukraine kutoka kwa nchi za Magharibi.

Baerbock amerudia miito ya Ujerumani kwa washirika wake watume mifumo zaidi ya ulinzi wa anga huku Urusi ikiishambulia Ukraine kwa makombora, mabomu na maroketi.

Ujerumani ni nchi ya pili inayopeleka msaada wa kijeshi Ukraine baada ya Marekani. Shirika la habari la Ujerumani dpa limeripoti kwamba Baerbock alikuwa amepangiwa kusafiri kwenda Kharkiv hivi leo lakini ziara yake ikafutwa kwa sababu za kiusalama.

Wakati hayo yakiarifiwa rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy amesema vikosi vya Urusi bado vinaelekeza nguvu katika mkoa wa mashariki wa Donetsk na eneo la kaskazini mashariki la Kharkiv, ambako mabomu yanasababisha uharibifu mkubwa kwa maeneo ya jeshi na raia.