Trump na Putin kukutana uso kwa macho
16 Julai 2018Usalama umeimarishwa mjini Helsinki nchini Finnland kufuatia mkutano wa kwanza wa kilele kuwahi kufanyika kati ya rais wa Marekani Donald Trump na Vladmir Putin wa Urusi. Polisi wametawanywa katika barabara zinazozonguka eneo zima la maakaazi ya rais wa Finland ambako mkutano huo utafanyika.
Wanajeshi wameweka vizuizi kwenye barabara zinazoelekea kwenye makaazi ya rais ambako mkusanyiko mkubwa wa tu unatarajiwa baadae kufika kutazama misusruru ya magari ya marais wa Marekani na Urusi watakapowasili katika eneo hilo kwa ajili ya mkutano huo wa kilele.
Saa chache kabla ya mkutano huo unaofuatiliwa kwa karibu na viongozi wengi wa dunia tayari rais Trump ameilaumu Marekani na sio Urusi katika suala la kuingilia uchaguzi wa nchi yake au katika suala la kunyakuliwa kwa jimbo la Crimea. Trump amesema kupitia ujumbe wa Twita aliyoiandika leo asubuhi akiwa hukohuko Helsinki kwamba uhusiano wa Marekani na Urusi haujawahi kuwa mbaya lakini amelaumu kwamba kwa miaka mingi Marekani imekuwa mpumbavu na sasa hivi inamtafuta mchawi.
Mkutano wa leo(16.07.2018) umekosolewa kabla hata haujaanza na wanasiasa katika bunge la Marekani kutoka nyama vyote baada ya Marekani wiki iliyopita kuwashitaki maafia 12 wa kijaasusi wa Urusi wanaotuhumiwa kuhusika na kitendo cha kudukua taarifa za chama cha Democrats katika uchaguzi wa mwaka 2016 ili kumsaidia Trump katika kampeini ya kugombea urais. Leo hii Trump ana kutana uso kwa macho na rais Putin kiongozi wa kiimla ambaye Trump ameshaonesha kwamba anamkubali.
Trump ambaye amekuwa akijaribu kushusha matarajio kuhusu kile kinachoweza kufikiwa katika mkutano huo amewaambia waandishi habari wakati akipata kiamsha kinywa leo asubuhi pamoja na rais wa Finnland kwamba anafikiri mkutano wake na Putin utakwenda vizuri.Pamoja na kauli hiyo kuna masuali mengi ambayo yamejitokeza kuhusu ikiwa kweli Trump ataweza kuikosoa kwa maneno makali hadharani Urusi kutokana na uingiliaji wake katika uchaguzi wa Marekani ambao umechochea kuundwa kwa jopo maalum la uchunguzi ambalo Trump mwenyewe ameliaita jopo hilo kuwa la kumtafuta mchawi.
Kupitia Twitta Trump amekuwa akionekana kuzidi kuhujumu harakati za uchunguzi na kumlaumu mtangulizi wake Barack Obama kwa kushindwa kuzuia juhudi za Urusi kuingilia uchaguzi wa mwaka 2016.Wakosoaji wa Trump na hata washauri wake wamemtolea mwito rais huyo kutumia mkutano huu kumshinikiza Putin kuhusu suala hilo la kuingilia uchaguzi pamoja na vitendo vingine vya uovu vya Urusi.Kadhalika suala la Syria linategemewa kuzungumziwa huku ukiwepo uwezekano wa kufikiwa makubaliano ambayo huenda Urusi ikaridhia kusaidia kusimamia kuondowa wanajeshi wa Iran na wapiganaji wa Hezbolla katika maeneo ya mpaka wa Syria na Israel.
Mwandishi:Saumu Mwasimba
MhaririJosephat Charo