Papa afikisha ujumbe wa amani na mshikamano Algeria
13 Aprili 2026
Uwepo wa Papa Leo mjini Algiers, Algeria ndio mwanzo wa ziara yake ya siku 11 itakayomfikisha katika mataifa mengine matatu ya Bara la Afrika ikiwa ni pamoja na Cameroon, Angola na Equatorial Guinea. Papa ameingia kwenye historia ya kuwa kiongozi wa kwanza mkuu wa kikatoliki kufanya ziara iyo kubwa barani Afrika.
Kiongozi huyo wa kiroho yupo Algeria na ujumbe wa kuishi pamoja na kuvumiliana kati ya mataifa yaliyo na waislamu na wakristo walio wengi, hasa katika kipindi hiki cha migogoro na pia kumuenzi mtakatifu Agostino aliyechangia safari ya kidini ya Papa Leo.
Trump amkosoa Papa hadharani
Lakini ziara hiyo ilianza kwa maneno makali kati ya Rais wa Marekani Donald Trump na Papa huyo, aliyezaliwa katika jimbo la Chicago, Marekani. Trump alianza kwa kumwambia Papa aache kuukingia kifua utawala ulio na itikadi kali na unaotaka kumiliki silaha za nyuklia, akisema Papa ni dhaifu na ni mtu asiyejiamini kuhusu kusitisha uhalifu.
Papa nae akajibu vikali kauli hiyo akisema amani na maridhiano ni mambo yanayohimizwa katika injili, akisisitiza kwamba injili haihubiri vita na kamwe hauogopi utawala wa rais Trump na wala hana hofu ya kusema kile Injili inalohimiza. Trump amekuwa akimkosoa Papa kwa kutoa wito wa kumalizika kwa mgogoro wa Mashariki ya Kati.
Papa leo aomba amani itawale dunia
Baada ya Papa kuwasili Algiers pia alisisitiza uwepo uo huo wa amani kwa walgeria, walipigania uhuru kutoka kwa Ufaransa, uliopatikana mwaka 1962.Maelfu kwa maelfu waliuwawa wakati huo, wakati vikosi vya ufaransa vilivyowatesa wafungwa na wengine kupotea kama sehemu ya kutaka kuendelea kuliongoza taifa hilo.
Baadae Papa atakutana na rais wa Algeria Abdelmadjid Tebboune pamoja na viongozi wengine. Papa aliwapongeza raia wa taifa hilo kwa heshima na umoja walionao, akisema hilo ndilo linalohitajika kwa sasa kuliko wakati mwengine wowote hasa wakati dunia ikiandamwa na matukio ya ukiukwaji wa sheria za kimataifa na tabia za ukoloni mambo leo.
Papa Leo hakutoa mifano lakini amekuwa akizungumzia kwa uwazi vita vya Urusi na Ukraine, vita vya Iran na hata uvamizi wa Israel Kusini mwa Lebanon.
Wasiwasi Camroon kuelekea ziara ya Papa
Huku hayo yakiarifiwa kuna minon'gono yanayoendelea nchini Cameroon ambayo ndio nchi ya pili papa atakayoitembelea ikiwa ni sehemu ya ziara yake barani Afrika.
Wakatoliki wa taifa hilo wanadai kuwa huenda ziara hiyo ikammpa nafasi Rais wa miaka mingi Paul Biya, kusafisha jina lake ikiwa ni miezi sita baada ya kutangazwa mshindi wa uchaguzi uliokuwa na utata.
Papa Leo atakutana na Biya siku ya Jumatano na tayari picha zinazomuonesha Papa akiwa amesimama karibu na rais Biya aliye na miaka 93, zimebandikwa kote mjini Yaounde.